KAMPUNI ya Uchimbaji madini ya dhahabu Geita (GGML) imetunukiwa tuzo ya Usalama ya Dunia ya 2021 kwa mwaka wa tatu mfululizo na kuifanya kampuni hiyo kuwa moja ya makampuni yanayofanya shughuli za uchimbaji wa madini kwa kuzingatia usalama mahala pa kazi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Tuzo hiyo imeendelea kuongeza rekodi kwa GGML ambayo pamoja na mambo mengine ilishinda tuzo kwa kufanikiwa kuzuia vifo kutokana na shughuli hizo za uchimbaji kwa miaka tisa na majeruhi kwa miaka miwili mfululizo (2020-2021).
Pia imekuwa kampuni ambayo inazingatia utendaji bora zaidi kwa kufuata miongozo na itifaki za uchimbaji kwa asilimia 97.6.
Tuzo hiyo imetolewa hivi karibuni na Kampuni mama ya Anglogold ambayo inamiliki migodi mbalimbali katika mabara manne duniani.
Akipokea tuzo hiyo Makamu Rais wa Anglogold katika nchi za Tanzania na Ghana, Simon Shayo amesema tuzo hiyo ni kielelezo cha umakini na weledi wa wafanyakazi wa GGML, wakandarasi na menejimenti katika kudumisha utamaduni wa usalama na uwajibikaji.
Alisema mafanikio hayo ya GGML yanajumuisha vipengele vitatu: kushirikisha watu katika kazi ya kujenga mazingira salama, kujenga mifumo imara inayosaidia kazi salama na kudhibiti hatari kupitia mifumo mbalimbali ya ngazi zote.
“Kuboresha mazingira ya usalama mahala pa kazi ndilo lengo muhimu zaidi la GGML, vile vile afya ya jumla na ustawi wa wafanyakazi wake ni jambo linalozingatiwa kwa sababu bila watu hakuna biashara lakini utu ni jambo linalokuja kwanza.
“GGML pia ilipata sifa kwa kuchukua hatua makini na za kiubunifu ili kuondoa na kudhibiti hatari zinazojitokeza mahala pa kazi,” alisema.
Alisema licha ya mafanikio hayo, GGML haitabweteka hivyo itajitahidi mara kwa mara kuhakikisha kuwa watu wote wanaoingia katika eneo lolote la kazi ndani ya kampuni hiyo wanarudi nyumbani salama baada ya kumalizika kwa zamu yao.
Alisema GGML itaendelea kufanyia kazi lengo la AngloGold Ashanti la 2030 la kutoa maeneo ya kazi yasiyo na madhara.
Leave a comment