KIKOSI dhidi ujangili kutoka Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori (TAWA) kimefanikiwa kumdhibiti fisi aliyemuua mtoto Kwangu Makanda (11) na kujeruhi watu wawili katika kijiji cha Mbogo wilayani Itilima Mkoani Simiyu. Anaripoti Christina Haule, Morogoro … (endelea).
Kaimu Kamishna Msaidizi Mwandamizi kitengo cha Mawasiliano ya Umma TAWA, Twaha Twaibu alisema walifanikiwa kumuua fisi huyo ili asilete madhara zaidi kwa binadamu kwa mujibu wa sheria ya Uhifadhi wa wanyamapori Namba 5 ya Mwaka 2009 ambayo inaruhusu kumuua mnyamapori yeyote anayehatarisha maisha ya binadamu
Alisema tukio la kuuawa kwa binadamu na wengine kujeruhiwa lilitokea tarehe 4 Oktoba mwaka huu, majira ya saa 6 mchana ambapo fisi huyo anaesemekana kutokea katika Pori la Akiba la Maswa alivamia makazi ya watu katika Kijiji hicho ambacho kipo karibu na hifadhi.
Twaibu alisema baada ya kupata taarifa ya tukio hilo haraka Meneja wa pori husika, Jonathan Musiba alituma askari wa Kikosi Dhidi Ujangili Maswa wakishirikiana na askari wa wanyamapori kwenda kumsaka na kumuua fisi huyo.
Aliwataja waliojeruhiwa na fisi huyo kuwa ni wanaume wawili ambao ni Fatili Lindai maarufu kwa jina la Tungu (43) na Miranda Sali maarufu kwa jina la Nyamoko (55)
Alisema majeruhi wote wamepelekwa na kulazwa katika hospitali ya Ikindilo wilayani humo kwa ajili ya matibabu huku hali zao zikiendelea vizuri.
Aidha TAWA imekuwa ikifanya jitihada kubwa kudhibiti wanyama hatari kwa ajili ya kuokoa maisha ya binadamu au kuzuia madhara ambayo yangeweza kusababishwa na wanyama hao.
Leave a comment