SHIRIKISHO la vyama vya wachimbaji wa Madini Tanzania (FEMATA) limetoa wito kwa Serikali kuunga mkono wazo la kuanzishwa kwa benki ya wachimbaji wadogo wa madini nchini ili itumike kusaidia kutatua changamoto sugu ya mkwamo wa mikopo pindi wanapohitaji kwa riba nafuu. Anaripoti Paul Kayanda, Mwanza … (endelea).
Wito huo umetolewa mwishoni mwa wiki na mmoja wa wajumbe wa mkutano mkuu wa FEMATA, Baraka Ezekiel katika kongamano la madini kitaifa lililofanyika jijini Mwanza.
Ezekiel amesema wachimbaji wengi hawaaminiki katika taasisi za kifedha huku sababu kubwa ikitajwa kuwa ni kutokuwa na mali zisizohamishika lakini pia ni watu wa kuhamahama pale yanapogundulika maeneo mapya ya uchimbaji wa madini hayo.
Mchimbaji huyo ambaye pia ni mmiliki wa kampuni ya Busolwa Mining ya Geita, amesema iwapo benki hiyo itaanzishwa tayari kuchangia mtaji wa Sh 200 milioni mpaka Sh 500 milioni.
“Kwa sababu nina uchungu kwa yale niliyoyapitia na sipendi nanyi wenzangu muyapitie ili mfanikiwe,” amesema.
Aidha, Baraka amesema wakipatikana wachangiaji 100,000, na kupata Sh 50 bilioni hali hiyo itawezesha kuwepo kwa benki hiyo na itasaidia ununuzi wa vifaa vya uchimbaji na utafiti wa maeneo yenye madini kupitia benki hiyo.
Pamoja na mambo mengine amemuomba Rais FEMATA, John Bina atengeneze kamati ya wachimbaji hao ili wazo hilo liwasilishwe kwenye wizara ya madini lipewe baraka kwa maana kuwa wizara ndiyo msimamizi mkuu wa wachimbaji na inafahamu changamoto zao.
Aidha, Bina naye ameunga mkono hoja hiyo na kutumia mwanya huo kuelezea changamoto zinazowatesa wachimbaji wadogo hasa ukilinganisha na utitiri wa kodi na tozo mbalimbali.
Kiongozi huyo amewataka wachimbaji hao kuunga hoja hii kwa nguvu kwa maslahi ya wachimbaji hao na Taifa kunufaika kwa ukuaji wa uchumi kupitia sekta ya madini.
Leave a comment