MFANYABIASHARA maarufu nchini, Rostam Azizi kupitia Kampuni yake ya Taifa Group, ameungana na kampuni ya Generation Capital Limited (GCL) kutoka Mauritius kuanzisha mradi wa mfumo wa uzalishaji wa umeme jua (photovoltaic) utakaogharimu dola za Marekani 140 milioni sawa na Sh. 330 bilioni. Anaripoti Gabriel Mushi …(endelea).
Mradi huo ambao awamu ya kwanza inatarajiwa kukamilika mwaka 2024, unatarajiwa kuzalisha megawati 180 ambazo zitawezesha Wazanzibar kuondokana na adha ya ukosefu wa nishati hiyo muhimu.
Taarifa iliyotolewa leo tarehe 15 Mei 2023 imesema kampuni hiyo ya GCL imesaini mkabata wa kihistoria na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) kupitia mpango wa mkataba wa ununuzi wa umeme (PPA).
Katika kutekeleza mradi huo kampuni hiyo ya GCL imeingia ubia na kampuni ya Kitanzania ya Taifa Energy ambayo ni moja ya kampuni zilizo chini ya Taifa Group inayomilikiwa na Rostam Azizi.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, mradi huo wa umeme jua utaanza kutekelezwa kwa awamu ambapo awamu ya kwanza ambayo itazalishaji Megawati 30, itatekelezwa katika eneo la Bambi katika ya wilaya ya kati iliyopo mkoa wa Unguja Kusini na kukamilika mwaka 2024.
Akizungumzia mradi huo, Mmiliki na Mwenyekiti wa Taifa Group, Rostam Azizi amesema mradi huo umedhihirisha malengo ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar katika kuzalisha nishati mbadala ambayo ni safi itakayosukuma gurudumu la maendeleo Visiwani humo na Afrika kwa ujumla.
“Kupitia ushirikiano huu Generationa Capital Limited, Taifa Group na SMZ utanufaisha visiwa vya Zanzibar kupata umeme wa uhakika na miundombonu bora ya uzalishaji ambayo itakuza uchumi wa Zanzibar na kuboresha maisha ya wananchi,” amesema.
Leave a comment