HOSPITALI ya Rufaa ya Sokoine mkoani Lindi, imesema chanzo cha kifo cha Rashid Akbar, aliyekuwa Mbunge wa Newala Vijijini, kilichotokea ghafla jana tarehe 15 Januari 2020, ni ugonjwa wa moyo. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Chanzo hicho kimetangazwa na Dk. Nicholas Mmuni, Kaimu Mganga Mfawidhi wa hospitali hiyo, baada ya mwili wa Akbar kufanyiwa uchunguzi kuhusu chanzo cha kifo chake.
Dk. Mmuni ameeleza kuwa, kabla ya umauti kumfika, Akbar alisumbuliwa kwa muda mrefu na maradhi ya moyo, na kupelekea kuwekewa mashine maalumu mwilini mwake, iliyokuwa inasaidia moyo wake kufanya kazi (Pacemaker).
“Baada ya mwili wake kupokelewa hospitalini hapa uchunguzi ulifanyika na kubainisha kwamba amefariki dunia kutokana na maradhi ya moyo yaliyokuwa yanamsumbua muda mrefu.
Ambayo yalipelekea kuwekewa mashine iliyokuwa inamsaidia moyo kufanya kazi vizuri, (pacemaker) ambacho alikuwa akitembea nacho ndani ya mwili wake siku zote, ameeleza Dk. Mmuni.
Marehemu Akbar alifariki dunia jana akiwa hotelini kwake Mingoyo iliyoko maeneo ya Mnazi Mmoja mkoani humo.
Mwili wake unatarajiwa kuzikwa leo tarehe 16 Januari 2020 majira ya saa saba mchana.
mungu amlaze mahali pema peponi ndugu yetu ”inna lilah wainna illah rajiunna”