SIKU chache baada ya Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kutengua zuio la kufanya mikutano ya hadhara kwa vyama vya siasa nchini, Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Mbeya, kimesema uamuzi huo umekuja wakati muafaka kwani pia ulikiathiri chama hicho tawala. Anaripoti Kenneth Ngelesi, Mbeya … (endelea).
Kauli hiyo imetolewa jana tarehe 6 Januari, 2023 jijini Mbeya na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Mbeya, Dk Stephen Mwakajumilo ambaye alisema zuio hilo lililokuwa limewekwa na Dk. John Magufuli, halikuwa na athari kwa vyama vya upinzani pekee bali hata kwa CCM.
Alesema kurudishwa kwa mikutano hiyo kuna nafasi kujadili masuala na maendeleo baina ya chama tawala na vyama vya upinzani.
Alisema mikutano ya hadhara ni haki ya kikatiba hivyo wanampongeza Rais Dk. Samia kwani uamuzi huo ni faida kwa chama chake na wao viongozi wamepata uwanja wa kueleza mambo mambo yaliofanywa na serikali
Aidha, aliongeza kuwa wakati fulani walikuwa wakivizia ziara za mawaziri au mikutano ya madiwani, wabunge na wakati mwingine waliwachia wabunge kuwaeleza wananchi miradi iliyofanywa na serikali lakini kwa sasa wamepata nafasi ya kueleza.
Kwa upande wake Katibu wa itikadi na ueneza CCM mkoa wa Mbeya, Bashiru Madodi alisema mbali na vyama vya upinzani pia CCM ndicho kitakachonufaika zaidi kwa kueleza shughuli za maendeleo zilifanywa katika kipindi cha zuio.
Naye mdau wa siasa mkoa wa Mbeya, Boniface Mwabukusi alisema hakukuwa na uhalali wowote wa kuzuia mikutano hiyo na kwamba katazo hilo lilikuwa haramu kwa mujibu wa katiba.
Leave a comment