MBUNGE Viti Maalum asiye na chama bungeni, Ester Bulaya, amehoji lini Serikali itapeleka maji katika vijiji vilivyopitwa na Mradi wa Maji wa Nyabehu mkoani Mara. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Mradi wa Nyabehu unaotoa maji katika Ziwa Victoria, kwenda Wilaya ya Bunda mkoani Mara, ulianza kutekelezwa mwaka 2006 hadi 2015, kwa gharama ya Sh. 10 bilioni, ambao ulifadhiliwa na Benki ya Dunia (WB), ikishirikiana na Serikali ya Tanzania.
Akizungumza bungeni jijini Dodoma, leo Jumatatu tarehe 31 Mei 2021, Bulaya amesema mkataba wa ujenzi wa mradi huo, unaelekeza ujenzi wa vituo vya maji katika vijiji 14 jirani na Nyabehu, ili vipate maji kabla haujafika Bunda.
“Mradi wa Bunda umechukua muda mrefu sana takribani miaka 13, lakini moja katika makubaliano kwenye mkataba wa mradi ule, ni kujenga vituo kabla mradi haujafika Bunda Mjini, kwenye eneo linalotoka Nyabeho,” amesema Bulaya na kuongeza;
“Nataka kueleza maeneo yanayopita mradi kama Kinyambwigwa, Tairo, Buta na Bunda Stoo, kabla haujafika center (kituoni). Lini mtaweka vituo ili wananchi wa maeneo yale wasisikie mradi unatoka chanzo cha maji jirani na kwao, halafu vijiji ambavyo vinapitia havijapata maji?” amesema Bulaya.
Akijibu swali hilo, Naibu Waziri wa Maji, Marryprisca Mahundi, amesema wizara hiyo italifanyia kazi suala hilo, ili vijiji tajwa vipate maji.
“Sisi kama wizara tayari tunaendelea kuona kwamba, maeneo ya miradi ambayo imekaa muda mrefu inakamilika. Na Sera ya maji inataka pale kwenye chanzo cha maji na kadri ambavyo mradi unakwenda, tunaendelea kusambaza maji,” amesema Mahundi na kuongeza:
“ Yule wa karibu na chanzo, ataendelea kupata maji wa kwanza kulikoni yule aliyeko mbali. Nikuhakikishie maeneo yote ambayo umeyataja, yatazingatiwa kuona kwamba maji yanafika.”
Mradi wa Maji wa Nyabehu unaotekelezwa na Kampuni ya Nyakirang’ani, ulisuasua kwa miaka kadhaa, kutokana na ukosefu wa fedha.
Leave a comment