MBUNGE wa Viti Maalum kupitia Chama cha Mapinduzi (CCM), Asha Abdallah Juma ameitaka Serikali ya Tanzania kueleza jinsi ilivyojipanga katika udhibiti wa ufanyaje wa biashara holela unaofanywa na wafanyabiashara ndogondogo ambao walipewa vitambulisho vya machinga. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea).
Katika swali la Asha aliloliuliza leo Jumanne tarehe 26 Mei, 2020 bungeni kwa njia ya kidigitali na kujibiwa kwa mfumo huo huo, amesema, zoezi la kuwapatia vitambulisho wajasiriamali wamachinga limefanyika vizuri na kuendelea kufanya biashara zao mahali popote.
“Je, Serikali imejipanga vipi ili kuhakikisha kuwa na usimamizi na udhibiti katika ufanyaji wa biashara holela,” amehoji Asha
Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tamisemi amesem, Serikali kupitia wizara ya fedha na mipango kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais – Tamisemi imetunga Kanuni za Usimamizi wa Kodi (Usajili wa Wafanyabiashara Wadogo na Watoa Huduma) za mwaka 2020.
Amesema, kwa mujibu wa kanuni hizo, mamlaka za serikali za mitaa zimeelekezwa kusimamia na kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara na watoa huduma wadogo ili kuhakikisha biashara holela zinadhibitiwa.
“Udhibiti na usimamizi utafanyika wakati wa kusajili na kuwapatia vitambulisho wajasiriamali wadogo kwa lengo la kuwawezesha kiuchumi na kuhakikisha wanaendesha shughuli zao pasipo kubugudhiwa.”
“Sambamba na kanuni hizo, Serikali imeandaa mwongozo wa usimamizi wa wafanyabiashara wadogo na watoa huduma wadogo ambao umeainisha majukumu ya kila mdau katika usimamizi wa wafanyabiashara wadogo na watoa huduma wadogo,” amesema waziri huyo katika majibu yake
Leave a comment