BARAZA Kuu la Waislamu Tanzania (Bakwata) limewataka waumini wake na watanzania wote nchini kumpuuza mtu mmoja aliyejitokeza huko mkoani Pwani, akidai kuwa yeye ni Nabii Ilyasa, anaandika Irene David.
Mwenyekiti wa Halmashauri BAKWATA taifa na Msemaji Mkuu wa Mufti, Khamis Mataka, amethibitisha kuwepo na upotoshwaji wa mafundisho ya Uislamu yatolewayo na Hamza Issa, “Mtume Ilyasa” wakati akizungumza na waandishi wa habari katika makao makuu ya baraza hilo jijini Dar es Salaam.
Issa anadai kuwa yeye ni Muislam amepewa ufunuo na kwamba roho ya ”Mtume Ilyasa” imemuingia na hivyo yeye ndiye “Nabii Ilyasa” mwenyewe.
Anatumia Qurani na mafunzo ya kiislamu jambo lililosababisha Baraza la Masheihk wa mkoa wa Pwani kutolifumbia macho na kuleta maazimio yao kwa Mufti Mkuu.
Kwa mujibu wa Imani yetu sisi Waislam, tunaamini kuwa hakuna Nabii aliyekuwepo na atakaye kuja kuwepo tena zaidi ya Nabii na Mtume Mohammad.
Leave a comment