WAKATI Mamlaka nchini Kenya, ikiendelea kukabidhi miili ya watu waliofariki kutokana na njaa baada ya kupokea maelekezo ya mchungaji mwenye utata Paul McKenzie, aliyewaagiza kufunga hadi kufa ili wakutane na Mungu, baba wa familia moja amejitokeza kuomba msaada ili kuzika miili wa watu wanne wa familia yake. Inaripoti Mitandao ya Kimataifa … (endelea).
Hatua hii inakuja ikiwa ni mwaka mmoja tangu kugunduliwa kwa makaburi ya pamoja kwenye msitu wa Shakahola, Pwani ya Kenya ambapo jumla ya watu 429 waliripotiwa kupoteza maisha.
Zoezi la kugawa miili 34 iliyotambuliwa na ndugu zao, limeanza jana Jumanne tayari saba imekabidhiwa kwa familia tatu kwa ajili ya mazishi baada ya kupewa ushauri wa kisaikolojia na wanachama wa kamati ya kimataifa ya msalaba mwekundu.
Mmoja wa familia hizo tatu ni Titus Ngonyo aliyesema katika janga hilo amempoteza mke, mtoto, mjukuu na mkwewe huku mjukuu mwingine akinusurika.
“Tumezidiwa, tuna mawazo mengi na tumeamua kuwazike wote wanne hao kwenye kaburi la pamoja nyumbani kwetu. Lakini tunahitaji msaada wa haraka kutoka kwa Serikali kwani hatuna hata hela za kununua jeneza moja
“Imekuwa safari ndefu. Angalau, nitakuwa nao karibu. Tunapanga kuwazika kwenye kaburi la pamoja karibu na nyumba yangu,” alisema Ngonyo.
Alisema familia imepata msiba mkubwa kwa kuondokewa na mkewe, mwanaye Isack, mkwewe Emily Wanje na mjukuu Seth Ngala aliyekuwa na umri wa miaka mitano.
Alieleza kuwa jitihada zake za kumshawishi mkewe asijiunge na kanisa hilo la Good News International Church, ziligonga mwamba.
Alisema mwanaye Isack Ngala, aliacha kazi jijini Nairobi mwaka 2019 kufuata mhubiri Mackenzie.
Mkewe Isaac, Emily pia aliacha kazi yake ya ualimu katika shule ya Malindi ili kujiunga na mumewe kwa mhubiri huyo
“Japo watu wanne wa familia yangu waliangamia katika janga la Shakahola, mjukuu mmoja, Ephraim, alinusurika mwaka jana,” alisema
Pia alisema mwanaye pekee aliyebakia William Ponda Titus, alikwepa janga hilo kutokana na kazi ya udereva aliyokuwa akiifanya mjini Mombasa.
Leave a comment