ASKOFU Mkuu wa Kanisa Katoliki Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Yuda Thadeus Ruwa’ichi amewaagiza mapadre wote wa jimbo hilo kupata chanjo ya ugonjwa wa corona (COVID-19). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Askofu Ruwa’ichi ametoa wito huo leo Jumanne, tarehe 24 Agosti 2021, katika Kituo cha Hija cha Pugu, jijini Dar es Salaam, wakati akihubiri kwenye adhimisho la misa takatifu ya mazishi ya Padri Paul Peter Haule.
Padri Haule aliyefariki dunia tarehe 18 Agosti 2021, kwenye Hospitali ya Kardinali Rugambwa, Ukonga, akipatiwa matibabu. Alikuwa Paroko Msaidizi wa Kanisa Katoliki, Parokia ya Mtakatifu Petro, Oysterbay mkoani Dar es Salaam.
Kiongozi huyo wa kiroho amesema, tayari Baba Mtakatifu Francis amekwisha kuonesha mfano wa kuchanjwa.
“Na kwa sababu hiyo, sijui mapadri wangapi ambao mmeshachanjwa, lakini leo naomba nitoe agizo kila Padri akachanjwe, tusifanye utoto, tusifanye lele mama hii Covid-19, haina mjomba na shemeji, inatuumiza,” amesema Askofu huyo
Askofu Ruwa’ichi amewaomba Watanzania wafuate ushauri unaotolewa na wataalamu wa afya, kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo.
“Tufuate maelekezo ya wataalamu, najua hiki ni kipindi ambacho kuna maneno mengi.”
“Naomba niwaambie kwamba hata waliotutangulia kuchanjwa ni Baba Mtakatifu Francis, ametupa mfano wa kuchanjwa yeye mwenyewe, mimi nimewapa mfano wa kutangulia kwenda kuchanjwa,” amesema Askofu Ruwa’ichi.
Leave a comment