ASASI za Kiraia nchini Tanzania (AZAKI), zimezindua mwongozi wa ulipaji kodi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar ea Salaam … (endelea).
Mwongozo huo umezinduliwa leo Ijumaa, tarehe 24 Septemba 2021 na Kaimu Naibu Kamishna wa Uchunguzi wa Kodi, kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Feliciana Nkane.
Uzinduzi huo, umefanyikia Ofisi za Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), mkoani Dar ea Salaam.
Akizungumza katika uzinduzi huo, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, amesema muongozo huo ni hatua muhimu katika kukuza uelewa na utekelezaji wa sera na sheria za kodi.
“Pamoja na hayo Asasi za Kiraia zimekuwa zikifanya manunuzi makubwa na pia kutoa huduma mbali mbali kama vile elimu, afya, utunzaji wa mazingira, utawala bora na shughuli zingine nyingi, ambazo zinachangia maendeleo ya kitaifa kwa ujumla.”
Kwa kifupi, mwongozo huu unaelezea namna ya kujisajiri kama mlipa kodi, matakwa ya sera, sheria na miongozo mbalimbali kuhusu haki na wajibu katika kulipa kodi,” amesema Olengurumwa.
Olengurumwa amesema “vilevile, mwongozo unaelezea dhana tofauti kuhusu aina tofauti za kodi ikiwa ni pamoja na ushuru na kodi mbalimbali. Ila mwongozo umeelezea ni kwa namna gani taasisi inaweza kuwa Taasis ya Kihisani (Charitable organization) na namna taasisi za kihisani zinatozwa kodi.”
“Kiujumla, mwongozo huu umejikita katika kuelezea maeneo ambayo yana changamoto katika ulipaji wa kodi kutoka Asasi a Kiraia ili kukuza uelewa na utekelezaji wa sera na sheria za kodi.”
Amesema mwongozo huo ni matunda ya warsha ya mafunzo mbalimbali ya kukuza uwezo wa asasi hizo katika utekelezaji wa miongozo ya kodi, ikiwemo ile iliyokutanisha wadau hao na TRA.
“Kwa kutambua umuhimu huu, July 2019, THRDC na washirika wake kwa kushirikiana na TRA iliandaa warsha na mafunzo mbalimbali ili kukuza uwezo wa Asasi za Kiraia katika utekelezaji wa sheria na miongozo mbalimbali ya kodi. Warsha na mafunzo haya yalipelekea kutengeneza rasimu ya Mwongozo wa Kodi kwa Asasi za Kiraia kama Jarida maalumu,” amesema Olengurumwa.
Olengurumwa amesema, THRDC kupitia wanachama wake itaendelea kutoa mchango serikalini.
“THRDC ni mwamvuli wa mashirika yasiyo ya kiserikali yanajishughulisha na utetezi wa haki za binadamu nchini Tanzania huku ukiwa na zaidi ya wanachama 200. THRDC kupitia wanachama wake imeendelea kuonesha mchango wake katika kutatua changamoto mbalimbali hapa nchini. Mtandao unatambua umuhimu wa wanachama wake katika ngazi mbalimbali kushirikiana na serikali katika kujenga nchi,” amesema Olengurumwa.
Kwa upande wake Nkane, amezipongeza asasi za kiraia kwa jitihada inazofanya kuchangia pato la taifa kupitia kodi mbalimbali kama vile Kodi ya Mapato (PAYE), Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT), Withholding Tax (Kodi ya Zuio) , Kodi ya Mhuri (Stamp Duty) na kodi zingine nyingi.
Leave a comment