CHAMA cha ACT-Wazalendo, kimeiomba Serikali iweke mfumo utakaohakikisha asilimia 30 ya manunuzi ya bidhaa na huduma inazotumia, zinatoka kwenye biashara za wanawake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Ombi hilo limetolewa leo Jumanne, tarehe 8 Machi 2022, jijini Dar es Saalam na Msemaji wa Kisekta wa Ustawi wa Maendeleo ya Jamii, Wanawake na Watoto wa ACT-Wazalendo, Janeth Rithe, kupitia ujumbe wake wa maadhimisho ya siku ya wanawake duniani.
“Serikali iweke mifumo thabiti kuhakikisha angalau asilimia 30 ya manunuzi yote ya ndani, yatakayofanywa na Serikali Kuu na Serikali za Mitaa, yatatoka kwenye biashara zinazozomilikiwa na ushirika wa wafanyabiashara wadogo wadogo wanawake,” imesema taarifa ya Rithe.
Rithe ameiomba Serikali kuweka fursa sawa za uwakilishi na uongozi kwenye vyombo vya maamuzi, hususan katika nafasi za kuteuliwa.
“Serikali kusimamia hupatikanaji wa tume huru ya uchaguzi, ili kuhakikisha wanawake wanapata ujasiri wa kushiriki siasa. Kukomesha ajira za kingono na unyanyasaji wa kijinsia, maeneo ya kazi na kutambua biashara ndogondogo na kuziwekea utaratibu wezeshi wa kuendesha kwa kuondoa msururu wa kodi,” imesema taarifa ya Rithe.
Aidha, Rithe ameiomba Serikali na wadau waongeze juhudi za kutokomeza masuala ya ukatili wa kijinsia kwa wanawake, hasa mauaji ya imani za kishirikina na ukatili wa kingono.
“Mathalani, katika baadhi ya Mikoa hapa nchini wanawake Wazee bado wameendelea kuripotiwa kuuawa kwa imani za kishirikina, huku wanawake vijana wakiishia kufanyiwa vitendo vya kikatili na wengine kuuawa na weza au wapenzi wao kutokana na wivu wa mapenzi,” imesema taarifa ya Rithe.
Leave a comment