WAZIRI wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amesema kazi ya kuondoa tope inaendelea na shughuli kubwa inayofanyika kwa sasa ni kufungua mitaa yote ya mji wa Katesh na kurejesha mji katika hali yake ya awali kwa kuwezesha shughuli za uzalishaji kuendelea. Anaripoti Danson Kaijage, Kateshi (endelea).
Ameyasema hayo leo Jumatano wakati wakikagua kazi zilizofanyika huku akiwa ameambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Jenista Mhagama; Waziri wa Madini, Antony Mavunde na viongozi wengine.
“Maelekezo ya Rais Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha mji wa Katesh na mitaa yake inasafishwa ili shughuli za uzalishaji ziendelee,” amesema Bashungwa.
Bashungwa amesema Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) kwa kushirikiana na Wakala ya Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) tayari wameweka mpango kazi wa pamoja ambao utahakikisha kazi hiyo inaendelea kufanyika usiku na mchana mpaka shughuli hiyo itakapokamilika.
Aidha, Waziri Bashungwa amevipongeza vyombo vya ulinzi na usalama, kwa kazi kubwa wanayofanya ambapo wamehakikisha wanaleta vijana wa JKT wanaoshiriki katika zoezi la uokozi ikiwa ni pamoja na kusaidia kazi za kurejesha hali nzuri katika mji wa Katesh.
Naye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Jenista Mhagama amesema wanaendelelea kutekeleza maagizo ya Rais Samia ambayo kuhakikisha matibabu kwa waathirika wa maafa hayo yanatolewa bure.
Pia amesema wanaendelea kutafuta miili, kazi ambayo inaendelea na inafanywa na vikosi vya ulinzi na usalama na kuhakikisha wale ambao wameokolewa wanatayarishiwa maeneo ya kuishi na kupatiwa huduma nyingine za kijamii.
Leave a comment