Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua programu ya nishati safi ya kupikia itakayosaidia wanawake barani Afrika (AWCCSP) kesho Jumamosi katika Umoja wa Falme za Kiarabu- Dubai. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Marais wa nchi mbalimbali na viongozi wa ngazi za juu za serikali na mashirika ya kimataifa wamealikwa kuhudhuria uzinduzi wa programu hiyo yenye lengo la kuchangia upatikanaji wa nishati safi ya kupikia kwa nchi zilizo chini ya Jangwa la Sahara.
Takwimu zinaonesha kuwa zaidi ya watu milioni 900 kwenye nchi hizo hutumia kuni na mkaa kupikia jambo ambalo huathiri zaidi wanawake na watoto kwani ndio watafutaji na watumiaji wakubwa wa nishati hiyo.
Athari za matumizi ya nishati zisizo safi za kupikia ni pamoja na za kiafya, ambapo inaelezwa kuwa watu zaidi ya 500,000 kwenye ukanda huo hupoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa yatokanayo na matumizi ya nishati hizo.
Kwa upande wa athari za kimazingira, takwimu zinaonesha upotevu wa hekta milioni 3.9 za misitu kila mwaka kutokana na shughuli za ukataji misitu na hivyo kuongeza athari za mabadiliko ya tabianchi
Athari nyingine ni za kijamii ambapo wanawake na watoto hususani maeneo ya vijijini hukumbwa na vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia kutokana na kutembea umbali mrefu kutafuta kuni.
Aidha, kundi hili hukosa muda wa kutosha kujihusisha na shughuli za maendeleo kutokana na kutumia muda mrefu kutafuta kuni.
Akizungumza wakati wa kikao na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba amesema maandalizi ya uzinduzi yanaendelea na tayari baadhi ya marais na viongozi mbalimbali wamethibitisha ushiriki wao.
Rais Samia pia ameambatana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Selemani Jafo, Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega, mabalozi na maafisa mbalimbali wa Serikali, Katibu Mkuu wa Nishati, Mhandisi Felchesmi Mramba.
Uzinduzi wa program hiyo utafanyika wakati wa Mkutano wa 28 wa Mabadiliko ya Tabianchi wa Umoja wa Mataifa (COP28) utakaofanyika kuanzia tarehe 30 Novemba hadi tarehe 12 Desemba 2023 ambapo Marais zaidi ya 140 kutoka mataifa mbalimbali duniani na washiriki takriban 70,000 wanatarajiwa kuhudhuria.
Leave a comment