MAHAKAMA ya Hakimu Mfawidhi, wilaya ya Igunga, mkoani Tabora imemhukumu kifungo cha miaka mitatu gerezani, Jesca Jones Yegera (60) baada ya kupatikana na makosa mawili, kushawishi na kutoa rushwa. Anaripoti Abdallah Amiri, kutoka Igunga…(endelea).
Jessca amedaiwa kutoa rushwa ya Sh. 500,000 kwa Afisa Utumishi wa halmashauri hiyo, Erick Sije (38), mfanyakazi wa halmashauri ya wilaya ya Igunga.
Mahakama imesema, imeridhika na mashitaka yaliyowasilishwa mbele yake na upande wa mashitaka na hivyo, imemuona mtuhumiwa ana hatia kwa makosa aliyoshitakiwa nayo.
Mapema mwendesha mashitaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), wilayani Igunga, Mazengo Joseph, aliiambia Mahakama mbele ya Hakimu Mfawidhi wa wilaya, Edda Kahindi, kwamba Jesca alitenda makosa hayo, tarehe 24 Juni 2022, kwenye ofisi za halmashauri ya wilaya ya Igunga.
Alisema, mshitakiwa huyo alishawishi na kutoa rushwa ya Sh. 300,000 kati ya Sh. 500,000 alizoahidi kwa njia ya simu ili aweze kumsaidia kupata madai yake ya malimbikizo ya mishahara ya miezi mitano aliyokuwa anadai kutoka serikalini, kiasi cha Sh. 6,175,000.
Alisema mshtakiwa huyo alitenda makosa hayo mawili kinyume na kifungu cha 15 (1) (b) (2) cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa, Sura 329 mapitio ya 2019 inayozuia kutenda makosa ya aina hiyo.
Hata hivyo, baada ya kusomewa mashitaka hayo mawili, mshitakiwa alikana kutenda makosa hayo na ndipo upande wa mashitaka ulipeleka mashahidi sita kuthibitisha madai yao.
Baada ya kusikiliza ushahidi wa pande zote mbili, Hakimu Edda alisema ushahidi uliotolewa na Jamhuri umemuona Jesca ana hatia.
Hivyo Mahakama inamhukumu kulipa faini ya Sh. 1,000,000 na akishindwa kulipa atakwenda jela miaka mitatu ili iwe fundisho kwa watu wengine wenye tabia hiyo. Hadi mwandishi anaondoka mahakamani Jesca alikuwa hajaweza kulipa faini hiyo.
Leave a comment