JAJI Mkuu wa Tanzania, Prof. Ibrahim Juma, amesema tume mbalimbali zimeundwa kwa ajili ya kukusanya maoni kuhusu maboresho ya haki jinai, lakini mapendekezo hayo yamekwama kutekelezwa kwa sababu ya ukosefu wa rasilimali fedha. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Prof. Juma ametoa kauli hiyo leo tarehe 15 Julai 2023, akizungumza katika hafla ya Rais Samia Suluhu Hassan, kupokea taarifa ya tume aliyounda kuangalia jinsi ya kuboresha haki jinai nchini, Ikulu jijini Dar es Salaam.
“Tume ya Jaji Bomani mapendekezo mengi hayakufanyika kwa sababu ya ukosefu wa fedha, zilitakiwa dola za marekani 285 milioni, kutekeleza mapendekezo yote lakini kutokana na ukosefu wa fedha yakawa yanateklezwa vipande vipande ndiyo maana unakuta sehemu kubwa hayakutekelezwa,” amesema Prof. Juma.
Kutokana na changamoto hiyo, Prof. Juma amemuomba Rais Samia Suluhu Hassan, alitatue tatizo hilo kwa kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyotolewa na tume hiyo inayoongozwa na Jaji Mkuu Mstaafu, Othman Chande.
Naye Jaji Mkuu mstaafu wa Tanzania, Joseph Warioba, amesema mapendekezo hayo yakifanyiwa kazi itasaidia kuboresha utendaji wa taasisi za haki jinai nchini.
“Katika nchi yetu wakati wa amani sura ya dola ni vyombo vinavyoshughulika na haki jinai na mahakama na kazi waliyofanya itasaidia sana kwa wananchi kuelewa utaratibu wa haki jinai katika nchi yetu na pia itasaidia mahali ambapo tunahitaji kuimarisha ili vyombo hivi viweze kufanya kazi vizuri,” amesema Jaji Warioba.
Leave a comment