MAHAKAMA Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, imesimamisha Kwa muda usikilizaji wa kesi iliyofunguliwa na James Mbatia, kupinga kuvuliwa uanachama wa NCCR-Mageuzi, hadi Mahakama ya Rufani itakapotoa uamuzi dhidi ya rufaa iliyofunguliwa na Bodi ya Wadhamini ya Chama hicho, kupinga ufunguaji wake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Amri hiyo imetolewa leo tarehe 13 Julai 2023, mahakamani hapo mbele ya Jaji Abdi Kagomba, wakati akitoa uamuzi mdogo dhidi ya maombi yaliyowasilishwa na Wakili wa Bodi hiyo, Hassan Ruwanya, kuomba kesi ifutwe hadi rufaa Yao itakapoamuliwa.
Mbatia amefungua kesi hiyo Na. 18/2023 dhidi ya Bodi ya Wadhamini ya NCCR-Mageuzi, kupinga uamuzi wa Chama hicho kumfukuza pamoja na kumuondoa katika wadhifa wake wa uenyekiti Taifa, akidai mchakato uliofikia uamuzi huo haukuwa halali.
Akitoa uamuzi wa kusitisha Kwa muda kesi hiyo, Jaji Kagomba alikataa ombi la NCCR-Mageuzi lililotaka kesi ifutwe akisema hatua hiyo itaathiri haki ya mleta maombi pamoja na kumpa gharama za kufungua tena pindi rufaa itakapotolewa uamuzi na kumpa ushindi.
“Njia sahihi kwa pande zote mbili ni kusimamisha hadi hapo maamuzi ya Mahakama ya Rufani yatakapotolewa kwenye shauri Na. 512/2023, lililowasilishwa na wajibu maombi,” amesema Jaji Kagomba.
Jaji Kagomba ameamua kusimamisha usikilizaji wa kesi hiyo akisema endapo akikubali ombi la Mbatia kuendelea na usikilizaji wake, itasababisha mgongano wa maamuzi ya kisheria endapo Mahakama ya Rufani itaamua kwamba kibali alichopewa mwanasiasa huyo kufungua kesi, kilikuwa batili.
Bodi ya Wadhamini ya NCCR-Mageuzi, iliwasilisha rufaa Na. 512/2023 katika Mahakama ya Rufani, kupinga uamuzi uliotolewa na Jaji Leila Mgonya, katika Kesi Na. 4/2023 uliomruhusu Mbatia kufungua kesi ya kupinga kufukuzwa ndani ya chama hicho.
Katika kesi hiyo Na. 4/2023, Mbatia alikuwa anaomba kibali Cha kufungua maombi ya mapitio ya mahakama dhidi ya mchakato uliotumika kumng’oa NCCR-Mageuzi, kama ulikuwa halali au batili.
Mwanasiasa huyo alidai mchakato huo ulikuwa batili kwa madai kuwa hakupewa nafasi ya kusikilizwa na mkutano Mkuu unaodaiwa kufikia uamuzi huo kutokuwa halali.
Ambapo mahakama mbele ya Jaji Mgonya ilimpa kibali cha kufungua kesi ambayo kwa sasa imesimamishwa.
Hadi sasa haijajulikana rufaa iliyokatwa na Bodi ya Wadhamini ya NCCR-Mageuzi, itaanza kusikilizwa kutokana kwamba Wakili wa Mbatia, Hardson Mchau, anadai hajapewa wito wa mahakama dhidi yake.
Leave a comment