MKUU wa Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga, Festo Kiswaga amesema siri ya Manispaa ya Kahama kuwa mshindi wa kwanza kitaifa katika kilele cha mbio za Mwenge mwaka huu kwa miradi yake ni viongozi manispaa hiyo kuwa na umoja na mshikamano na juhudi ya nguvu za wananchi. Anaripoti Paul Kayanda, Chato … (endelea).
Kiswaga ametolea kauli hiyo leo tarehe 16 Oktoba, 2021 baada ya Waziri wa Nchi ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia sera, Bunge Ajira kwa Vijana na wenye Ulemavu, Jenista Mhagama kuitanga Manispaa ya Kahama kuwa mshindi wa jumla katika kilele cha maadhimisho ya mbio za mwenge wa Uhuru kitaifa yaliyofanyika wilayani Chato Mkoani Geita.
Kiswaga alitumia fursa hiyo kuwapongeza watendaji wa halmashauri hiyo na kuwasihi wazidi kuwa na ushirikiano kama huo ili kufanya shughuli za maendeleo kwa wananchi.
“Naomba wananchi wa Kahama mtembee kifua mbele tumehakikisha miradi yote inakuwa na tija lakini niwashukuru madiwani kwani ndiyo wamefanya kazi kubwa ya kusimamia rasilimali hizo na kuhakikisha kuwa fedha zinazoletwa na serikali zinafanya kazi iloiyokusudiwa,” amesema DC Kiswaga.
Mkuu huyo wa Wilaya amewaahidi wananchi wake kuwa atawashirikisha kwa kila kitu ili awamu nyingine wapate ushindi huo.
Amesema Rais Samia Suluhu Hassan kwa kipindi hiki ameleta fedha nyingi ambazo ya kimkakati watashirikiana na wananchi wa wilaya ya Kahama.
Naye Mbunge mteule wa Ushetu, Emmanuel Charahani amesema akiwa mmoja wa wajumbe wa baraza la madiwani atahakikisha wanamuunga mkono mkuu wa wilaya ili kuwaletea maendeleo wananchi.
Aidha, Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko amezitaka halmashauri za mkoa wa Shinyanga zisijivunie ushindi huo badala yake viongozi wote washirikiane katika kubuni vyanzo vya mapato licha ya kutegemea fedha za serikali.
Amesema Mkoa wa Shinyanga unaraslimali nyingi zinazoweza kufanya ushindi huo uzidi kubaki katika wilaya za Shinyanga.
Leave a comment