SAMIA Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, ameiagiza Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kupunguza viwango vya riba vinavyotozwa na benki mbalimbali zipunguzwe “angalau ziwe chini ya asilimia 10.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Amesema, hatua hiyo itapunguza machungu kwa wananchi ambao wamekuwa wakikutana na viwango vikubwa vya riba hivyo kuchelewesha maendeleo.
Rais Samia, ametoa maagizo hayo leo Jumapili, tarehe 13 Juni 2021, wakati akifungua jengo la Benki Kuu ya Tanzania, tawi la Mwanza.
“Benki Kuu iangalie riba isiwe inayomuumiza mwananchi, kwani zipo juu na naelekeza zianze kushushwa na kama mfumo una matatizo ushughulikiwe angalau uwe kuanzia asilimia 10 kwenda chini,” amesema Rais Samia.
Katika kusisitiza hilo, Rais Samia amesema “BoT iweke mikakati ya kuhamisha na kuweka mazingira Rafiki ya kutoa mikopo.”
Pia, ameelekeza Benki Kuu, ikaelekeza “nguvu katika kuhamisha matumizi ya mtandao ili kupunguza matumizi ya fedha taslamu. Itarahisisha biashara, makusanyo ya mapato na uchapishaji wa fedha.”
Rais Samia, ameagiza kuwapo kwa kanzidata mbili za kutunza taarifa “ya kwao yenyewe na nyingine itunzwe kwingine, ili moja inapoleta shida nyingine inafanya kazi. Nashauri BoT mshirikiane na wadau wengine ikiwemo wizara ya teknolojia ya habari, kuona jinsi ya kupata huduma hii kwa gharama nafuu.”
Katika uzinduzi huo, Rais Samia ameshitushwa na gharama za ujenzi wa jengo hilo lililogharimu Sh.42 bilioni ikiwa ni ghama za ujenzi na ufungaji wa vifaa vikiwemo vya ulinzi.
“Naipongeza sana Benki Kuu kwa jengo hili la kisasa, lakini ujenzi wa majengo haya gharama kidogo, zimesisimua mishipa ya fahamu, tutalitizama zilivyokwenda, leo ni uzinduzi na tutaulizana zimetumikae baadaye,” amesema
Awali, Gavana wa BoT, Profesa Florens Luoga amesema, kwa sasa benki hiyo, ina matawi manne- Mbeya, Mwanza, Mtwara na Arusha huku ikiwa na ofisi ndogo, Dar es Salaam na Zanzibar. Makao Makuu yamehamia Dodoma kuanzia Novemba 2020.
Amesema, ujenzi wa ofisi hizo ulifanyika “kutokana na kupanuka kwa majukumu ya BoT kanda ya ziwa na bodi ya wakurugenzi waliithinisha ujenzi wa jengo hili ambao ulianza Juni 2015 na kukamilika Ooktoba 2020.”
Amesema, baada ya kupitia ujenzi wa jengo, kulionekana kuna haja ya kuongeza ulinzi na kuanzia Aprili 2021, tulianza kuhamishia ofisi humu.
“Ujenzi umegharimu Sh.42.1 bilioni ikiwemo ufungaji wa vifaa mbalimbali ikiwemo mitambo ya usalama na mawasiliano,” amesema Profesa Luoga.
Gavana huyo amesema, BoT imekuwa inakutana na changamoto kadhaa ikiwemo “
“matumizi makubwa ya fedha taslimu katika kufanya miamala.”
Serikali inabidi angalie kwa jicho la pili je kweli hizo fedha zilitumika ni sahihi au laaa?