Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Kilimanjaro imemhoji Mbunge wa Same Magharibi (CCM), Dk.Mathayo David Mathayo kwa tuhuma za kukiuka sheria za uchaguzi kwa kuingiza magari 10 maalum ya kubebea wa gonjwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kilimanjaro…(endelea)
Mkuu wa Takukuru Mkoa wa Kilimanajro, Fidelis Kalungula amesema tarehe 7 Julai 2020 walipata taarifa za uingizwaji wa magari 10 katika jimbo la Same ambapo walifuatilia kwa ukaribu na kuthibitisha kuingia kwa magari hayo na kisha kuyakamata.
“Mnamo tarehe 7 mwezi huu tulipata taarifa kuna magari 10 yanakuja Kilimanjaro ambayo yanadhaniwa ni ya mbunge aliyekuwa madarakani na kwamba yamekuja kwa nia ya kuvunja sheria na makatazo yaliyopo katika sheria ya gharama za uchaguzi hivyo tulichokifanya hatua ya kwanza ili tupate ushahidi ni kuyashikilia hayo magari na mpaka sasa tunayashikilia,”amesema Kalungula
“Bado tunaendelea kuyashikilia magari hayo kwa ajili ya kupata ushahidi, kwamba je ni kweli ujio wa magari hayo yana uvunjifu wowote wa makatazo ya sheria ya Takukuru namba 11 ya mwaka 2007? tunaendelea na uchunguzi wa jambo hilo na baadhi ya watu wengine tumeshawaita watupe ufafanuzi ili kusudi siku ya mwisho tuwe na usahihi wa jambo hilo,” amesema
Aidha amesema magari hayo 10 yalikuwa yameandikwa kuonyesha yanaenda kata mbalimbali zilizopo jimboni kwa mbunge huyo hivyo wanaendelea na uchunguzi ili ukweli upatikane na kwamba hawatamwonea yoyote au kwenda kinyume na sheria inavyowaongoza.
Leave a comment