HATUA ya Bajeti ya Elimu kupungua siku hadi siku, imelalamikiwa na wadau wa elimu nchini. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Akizungumza na waandishi wa habari Prof. John Kalage, Mkurugenzi Mtendaji wa Hakielimu amesema kuwa, bajeti ya maendeleo ya elimu imeendelea kuwa ndogo ambapo sasa, Wizara ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) imetengewa asilimia saba pekee kwenye sekta hiyo.
“Kuna changamoto kadhaa ambazo zinaikabili sekta ya elimu, changamoto hizo zinatokana na kutokuwepo bajeti ya kutosha kwenye sekta hii. Ndio maana maoni yetu tunayatoa wakati huu wa upangaji wa bajeti,” amesema.
Amesema kuwa, wakati udahili wa wanafunzi unaongezeka kwenye shule za msingi kwa asilimia 17, idadi ya shule imeongezeka kwa asilimia moja tu tangu 2016.
“Katika ripoti ya CAG 2016/17 ilionesha, kulikuwa na upungufu wa madarasa kwa asilimia 85 na asilimia 83 kwenye matundu ya vyoo, na asilimia 66 kwenye nyumba za walimu, huu ni upungufu mkubwa sana.
“Lakini kwa sekondari kuna upungufu asilimia 52 ya madarasa na asilimia 84 ya maabara na 86 ya madawati, 85 ya nyumba za walimu na 88 mabweni na 53 ya mashimo ya choo jambo hili linashtua sana.
“Tunalo jukumu la kuishauri serikali kuwashauri wabunge na kupendekeza njia sahihi ya kufikia malengo, ambayo serikali imeweka ili kufanikisha utoaji wa elimu bure,”amesema.
Kalage amesema, HakiElimu inapendekeza serikali iangalie uwiano wa bajeti ya sekta ya elimu, kutokana na kushuka na kupungua kwa bajeti kuu chini ya viwango vinavyokubalika kikanda, kimataifa vikiwemo vilivyowekwa kwenye tamko lililotolewa nchini Korea 2015 linalotaka Nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara kutenga angalau asilimia 20 ya bajeti ya serikali kwenye sekta ya elimu.
“Uwiano wa bajeti ya elimu kwa bajeti ya serikali ukijumlisha na deni la taifa, umepungua kutoka asilimia 16.1 kwa mwaka 2016/17 hadi kufikia asilimia 15 kwa mwaka 2017/18 na kushuka zaidi kwa asilimia 14 kwa mwaka 2018/19, kama serikali ingezingatia makubaliano ya kimataifa, sekta ya elimu ingepata nyongeza ya bajeti ya Bil 4,666” amesema.
Leave a comment