ZITTO Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini, anahofia usalama wa maisha yake, kufuatia vitisho anavyopokea kutoka kwa baadhi ya wanasiasa, kutokana na hatua yake ya kuishawishi Benki ya Dunia (WB), kutoipa Tanzania fedha za mikopo Dola za Marekani 500 milioni. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Zitto ametoa kauli hiyo hivi karibuni katika mahojiano yake na Idhaa ya Kiswahili ya Amerika (VOA).
Zitto amesema anachukulia kwa uzito vitisho kutoka kwa wanasiasa hao, huku akitolea mfano tukio la kushambuliwa kwa risasi, Tundu Lissu, Makamu Mwenyekiti wa Chadema.
“Ninachukulia vitisho hivi kwa umakini sana sababu tuna mfano kutoka kwa mwenzetu Tundu Lissu aliyepigwa risasi, ambaye kwa sasa yuko Ubelgiji,” ameeleza Zitto katika mahojiano hayo.
Hata hivyo, Mwanasiasa huyo ambaye kwa sasa yuko ughaibuni, amesema kuna njama zinapangwa za yeye kufunguliwa kesi ya takatishaji fedha, pindi atakaporejea nchini.
“Usishangae baadae kusikia nimekamatwa pindi nitakapokanyaga ardhi ya Tanzania, sababu serikali inatumia mashataka ya utakatishaji fedha ambayo hayana dhamana kuwaweka jela wakosoaji wake,” amesema Zitto.
Lissu aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, alishambuliwa kwa risasi na watu wasiojulikana mwezi Septemba mwaka 2017, mjini Dodoma. Hadi sasa mwanasiasa huyo amegoma kurejea nchini Tanzania kwa madai ya kuhofia usalama wa maisha yake.
Kabla ya kushambuliwa kwa risasi, Lissu aliwahi kulalamika juu ya vitisho na matukio yaliyokuwa yanahatarisha usalama wa maisha yake, ikiwemo nyendo zake kufuatiliwa na watu wasiojulikana.
Kabla hajaenda ughaibuni, Lissu alikuwa mkosoaji mkubwa wa serikali, ikiwemo katika suala la ununuzi wa ndege kwa ajili ya kuboresha Shirika la Ndege la Taifa (ATCL).
Leave a comment