WATU wenye ulemavu nchini wameiomba serikali na taasisi mbalimbali binafsi kuwasaidia eneo la kujenga ofisi ya kudumu. Anaandika Angela Willium
Wamesema wanahitaji ofisi kwa kuwa hivi sasa sehemu wanayotumia wameazimwa kwa muda na Msikiti wa Membe Chai uliopo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Taasisi ya Walemavu ijulikanayo kama MITWE, Habibu Hamimu amesema tatizo hilo la kukosa ofisi wamekuwa nalo kwa muda mrefu sasa.
Aliyasema hayo wakati akipokea msaada wa viti vya walemavu na baiskeli kutoka Taasisi ya Furaha ya Switzerland.
“Tunaiomba serikali na wana jamii watusadie eneo la kujenga ofisi ya kudumu kwani hapa tulipo ni jengo la Msikiti wa Mwembechai ambayo hata hivyo hiyo inavuja kipindi cha mvua na misaada tuyopokea ni mikubwa ikilinganisha na ofisi tuliyo nayo, ” amesema Hamimu
Kwa upande wake, Katibu wa chama hicho wilaya ya Kinondoni, Saidi Machaku amesema walemavu wanakabiliwa na changamoto nyingi ikiwemo suala la afya.
“Wazazi au walezi wanao ishi na watu wenye ulemavu tuna waomba muwe mna waleta walemavu wenzetu katika kupokea misaada badala ya kuwafungia ndani na hapa kuna mlemavu mmoja sijamuona nahisi wazazi hawajamleta kwa kuwa wanaona aibu kuja naye, ” amelalamika.
Leave a comment