WAKATI Serikali ikijinasibu kuwa nchini hakuna njaa, bado jamii imeendelea kulalamikia upandaji wa bei ya vyakula, anaandika Dany Tibason.
Kwa nyakati tofauti baadhi ya wakazi wa mji wa Dodoma wameitaka serikali kufanya jitihada za kuhakikisha bei ya vyakula kushuka bei hususani unga wa ugali pamoja na mahindi.
Naye Leah Mauza amesema kwa sasa bei ya vyakula inatishia amani kutokana na kupanda kwa bei ya vyakula huku hela ikiwa ngumu kupatikana.
Akizungumza na MwanaHALISI Online amesema kwa sasa unga wa ugali umepanda bei kutoka Sh. 2,000 kwa kila hadi kufikia Sh. 2,500.
“Kwa wiki moja iliyopita debe la mahindi lilikuwa likiuzwa kwa sh 28000 hadi 30,000 lakini kwa sasa debe la mahindi limepaa hadi kufikia kati y ash.34000 hadi 35000.
“Kwa sasa kisado cha viazi kilikuwa kikiuzwa kwa Sh. 30,00 hadi 40,00 lakini kwa sasa bei imepanda hadi kufikia kati ya 5,000 hadi 6,000 jambo ambalo ni hatari zaidi,” amesema Leah.
Naye ni mfanyabiashara wa chakula ambaye hakutaka jina lake litajwe amesema wanalazimika kupandisha bei ya vyakula kutokana na hali yenyewe ilivyo.
“Hatuwezi kufanya bishara ya hasara, kila mtu anajua kuwa hali ya hewa ilikuwa mbaya sana mvua haikunyesha ya kutosha hivyo kwa sasa tunalazimika kuuza unga wa ugali kwa bei ya juu maana kwa sasa unga unauzwa kwa bei ya juu kuliko mchele,” amesema.
Hata hivyo kwa upande wa akina mama lishe wamesema biashara imekuwa mbaya kutokana na kukosekana kwa wateja na wale ambao wanapatikana wanalalamika kwa madai kuwa bei ni kubwa.
Hata hivyo mama lishe huyo amesema kwa sasa wanalazimika kupunguza kipimo cha chakula katika sahani jambo ambalo linawafanya hata wateja kulalamika.