MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Mhandisi Benilth Mahenge, ameongoza mamia ya waombelezaji katika mazishi ya Twaha Mwaya, aliyekuwa Katibu wa Baraza la Waislamu (BAKWATA), Mkoa wa Dodoma. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Kwenye mazishi hayo, Mhandisi Mahenge amesisitiza Waislam na Watanzania kwa ujumla kuwa na tabia ya upendo, umoja na mshikamano.
Akitoa salamu za rambirambi Mhandisi Mahenge amesema, nchi haiwezi kuwa na maendeleo kama haitakuwa na watu ambao wamejenga tabia kuwa na upendo, amani, umoja na mshikamano bila kujali itikadi za dini wala vyama vyao vya siasa.
Amesema, nchi yenye kutaka maendeleo, lazima viongozi wake wajenge tabia ya kuwapenda wale wanaowaongoza ikiwa ni pamoja na kutambua kuwa, viongozi ni sehemu ya jamii katika kushirikiana kwenye mambo mbalimbali yakiwemo ya furaha na huzuni.
Antony Mavunde, Mbunge wa Dodoma Mjini akitoa neno kwenye msiba huo katika makaburi ya Ostabey, amesema kifo cha katibu huyo aliyekuwa akikaimu nafasi ya Katibu wa BAKWATA ni pigo kubwa kwa Waislam na Tanzania kwa ujumla.
Amesema, kiongozi huyo alikuwa mstari wa mbele katika kuupigania Uislamu ili usonge mbele, na si hivyo tu bali alikuwa kiongozi ambaye alitamani kuona jamii anayoiongoza ikiwa na maisha mazuri hususani katika amani, haki, upendo na mshikamano.
Alhaji Mustafa Shabani Rajabu, Sheikh wa Mkoa wa Dodoma amesema, wauminiwa dini hiyo wanatakiwa kuwa wacha Mungu wakati wowote, ili kuhakikisha wanakuwa kioo katika jamii inayowazunguka.
Leave a comment