SERIKALI kupitia Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imefunga laini za simu 975,041, zisizosajiliwa kwa mfumo wa alama ya vidole. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Akihojiwa na Televisheni ya Taifa (TBC), Mhandisi James Kilaba, Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, amesema laini hizo zilizimwa usiku wa jana tarehe 20 Januari 2020, siku ambayo ilikuwa ukomo kwa watu wasiosajili laini kwa mfumo huo, kukatiwa mawasiliano.
Mhandisi Kilaba ameeleza kuwa, laini hizo zilizofungwa ni za watu wenye namba za vitambulisho vya uraia, vinavyotolewa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA).
Amesema, laini hizo zimezimwa kwa makundi, ambapo kundi la kwanza ni laini 656,091 za watu wenye namba za NIDA ambao hawakujisajili, na kundi la pili ni laini 318,950 ambazo usajili wake wa awali ulikuwa na dosari, hivyo zilitakiwa kusajiliwa tena lakini wahusika waligoma kusajili.
“Wenye namba ambao idadi yao kwa ujuma ni 975,041, hawa tutawazimia leo (jana) kuanzia saa 4 usiku, hawa watu wamekuwa wakiitwa lakini hawajarudi. Hawana sababu ya msingi ya kutozimiwa laini zao leo (jana), “ ameeleza Mhandisi Kilaba.
Mhandisi Kilaba amesema, zoezi hilo ni endelevu, na kwamba laini zisizosajiliwa zitazimwa kwa awamu.
“Na baada ya kuzimia hawa, tunazima kidogo kidogo kwa sababu ya mambo ya kiutaalamu, sababu huwezi kuzima laini milioni 5 au 10 kwa wakati mmoja. Watakapoenda wengi zaidi hawawezi kujisajili hawezi kupata huduma,” amesema Mhandisi Kilaba.
Aidha, Mhandisi Kilaba amesema zoezi la usajili wa alama za vidole ni endelevu kwa wale watakaohitaji laini mpya za simu.
“Wewe ambaye unahitaji laini mpya utasajili, usajili haukuwekewa ukomo wa tarehe ya leo, bali uhuishaji wa laini za simu walizokuwa wanamiliki zamani ukomo wao ni leo. Usajili unaendelea kama ambavyo watu watakuwa wanahama kwenda kwenye umri wanaotakiwa kupata simu,” amesema.
Leave a comment