SHEIKH Ponda Issa Ponda, Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislam nchini, ameachwa na Jeshi la Polisi kwa dhamana. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Akizungumza na MwanaHALISI Online, Ibrahim Mkondo ambaye ni Katibu wa Sheikh Ponda amesema, Sheikh Ponda ameachwa leo tarehe 20 Julai 2020, mchana.
“Sheikh ametoka leo, ameambiwa kesho saa 2 anatakiwa kuripoti polisi,” amesema Mkondo.
Sheikh Ponda alikamatwa tarehe 11 Julai 2020, alipokuwa ofisini kwake katika Msikiti wa Bungoni, jijini Dar es Salaam kwa madai ya kuandika waraka wenye uchochezi.
Kwenye waraka huo uliosomwa na Sheikh Ponda Issa Ponda, tarehe 9 Julai 2020 jijini Dar es Salaam, miongoni mwa mambo yaliyomo kwenye waraka huo ni pamoja na kuitaka serikali kuhakikisha uchaguzi mkuu wa mwaka huu unakuwa huru na haki, pia umuhimu wa kuwa na Katiba Mpya.
“Kwa hakika maelezo yetu ya nini tunataka kwa taifa letu katika uchaguzi huu, yangekuwa na maana sana kama Taifa lingekuwa na Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Tume Huru ya Uchaguzi, vinavyotokana na Wananchi wenyewe,” alisema Sheikh Ponda.
Leave a comment