MWENYEKITI wa Kamati ya Uongozi ya Chama cha Wananchi (CUF), Julius Mtatiro amejibu uongozi wa CUF wilaya ya Ubungo, uliomvua uanachama, na kusema kuwa hatajishughulisha na tangazo hilo na siyo jipya kwake, yeye anaendelea na majukumu yake kama kawaida. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mtatiro ameandika katika ukurasa wake wa Facebook, kuwa hiyo siyo mara ya kwanza kwa kikundi hicho alichokiita cha kihuni kutangaza kumvua uanachama, hivyo hawawezi kumshughulisha wala kuwashughulisha wenzake wanaofanya majukumu yao kitaifa.
Katika waraka huo wa Mtatiro amesema anawasubiri wahuni hao watangaze kumfukuza mara ya tatu, ya nne, ya tano na ya sita, lakini hatashtuka. Soma zaidi walaka huo hapa chini.
Ndugu zangu.
Nimeona taarifa kwenye mitandao kuwa kuna watu wanajiita viongozi wa CUF wilaya ya Ubungo na kwamba ati wamenivua uanachama wa CUF.
Bila shaka hawa ni vijana wa Bwana Yule na wanatumika kututoa kwenye ajenda kubwa za kitaifa. Mwezi Disemba mwaka jana pia wahuni hao walitangaza ati wamenivua uanachama, tangazo lao la jana si jipya!
Mimi naendelea na majukumu yangu kama Kiongozi wa Juu wa chama anayetambuliwa na chama na vikao vya chama, na vitangazo hivyo vya wahuni haviwezi kunishughulisha wala kuwashughulisha wenzangu.
Nasubiri tangazo lingine la wahuni hao, la kunifukuza uanachama mara ya 3, ya 4, ya 5 na ya 6.
Hawatushughulishi kabisa maana dawa ya mgonjwa ni kumpa dawa tu.
Mtatiro J,
Mwenyekiti wa Kamati ya Uongozi Taifa,
The Civic United Front (CUF),
05 Machi 2018.
Leave a comment