MGOGORO mkubwa unafukuta kati ya serikali na viongozi wakuu wa madhehebu ya kiislamu mkoani humo. Anaripoti Mwandishi Wetu.
Mgogoro unatokana na hatua ya mkuu wa mkoa wa Rukwa, Joachim Wangabo, kuzuia ujenzi wa msikiti wa kisasa mkoani humo.
Wakizungumza baada ya kumalizika swala ya Ijumaa mwishoni mwa wiki, mmoja wa viongozi wa kiislamu mkoani Rukwa amesema, “serikali inawabagua waislamu na hivyo hawana imani nayo.”
“Tunabaguliwa na serikali. Hivyo basi, hatuna imani nayo. Tunanyanyaswa kwenye nchi yetu. Hatuko tayari kushirikiana na serikali inayotubagua,” ameeleza sheikh huyo kwa sauti ya hasira.
Ameongeza, “hata leo sikwenda kwenye kikao cha RCC (kamati ya ushauri ya mkoa). Siwezi kwenda kwa kuwa mkuu wa mkoa ambaye ndiye mwenyekiti wa kikao hicho, amewadhalilisha viongozi wangu wa kiislamu.”
Anasema, hawezi kwenda kwenye mkutano huo kwa kuwa mkuu wa mkoa amesheheni kiburi; ametaka waislamu wote kutohudhuria vikao vya kamati za kata na wilaya.
Kufuatia hatua hiyo, taarifa zinamnukuu kiongozi huyo wa kidini akiagiza waislamu wote kujiweka tayari, ili kutekeleza alichoita, “maelekezo” yatakayotolewa na viongozi wao wa misikiti.
“Kwa sasa, tulieni kidogo. Subiri mpaka Jumatano ijayo. Baada ya hapo, maimamu wenu watatoa kauli. Naomba ikitolewa hiyo kauli, mutekeleze mtakachoambiwa,” ameeleza.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, hatua ya mkuu wa mkoa huo kuzuia ujenzi wa msikiti na kutaka kubomolewa inafuatia madai kuwa umejengwa mjini na hivyo unaleta kelele kwa watu ambao siyo waislamu.
Leave a comment