KUELEKEA kufungwa kwa dirisha dogo la usajili, klabu ya Yanga imefanikiwa kumsajili mshambuliaji wa kimataifa kutoka Burundi, Fiston Abdul Razak ili kuongeza nguvu kwenye eneo la ushambuliaji. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Mshambuliaji huyo mwenye miaka 27, huenda akawa anafunga usajili ndani ya klabu hiyo kwenye dirisha dogo mara baada ya kufanikiwa kuwanasa Saidi Ntibazonkiza pamoja na Dikson Job kutoka Mtibwa.
Kupitia mitandao ya kijamii ya klabu hiyo ilimtambulisha Fiston kama mchezaji wao mpya mara baada ya kitendawili cha muda mrefu.
Uongozi wa klabu hiyo umeamua kufanya usajili wa mshambuliaji mara baada ya kutolizishwa na viwango vya washambuliaji waliopo kwa sasa licha ya timu hiyo kuongoza Ligi mpaka sasa na kutopoteza mchezo wowote.
Fiston ambaye ni mchezaji tegemeo kwenye timu ya Taifa ya Burundi ameshawahi kucheza kwenye klabu za Mamelodi Sundown ya Afrika Kusini na Sofapaka ya Kenya katika maisha yake ya mpira.
Kwa usajili huo huenda akaenda kuongeza nguvu kwenye eneo la ushambuliaji ambapo mara nyingi alikuwa akicheza Michael Sarpong ambaye ameonekana kutokuwa na makali.
DANIERY