WATUMISHI katika Kituo cha Ukaguzi Kibaha mkoa wa Pwani, wameondolewa kazini na serikali kutokana na kushindwa kusimamia rasilimali za sekta ya mifugo na uvuvi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Agizo hilo limetolewa leo tarehe 5 Desemba 2018 na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina katika kikao cha tathmini ya Operesheni Nzagamba awamu ya pili kilichofanyika jijini Dodoma.
Mpina amesema watumishi wasio waadilifu na kushindwa kutekeleza majukumu yao hawana nafasi katika Wizara yake, ndiyo maana ameagiza kuondolewa mara moja kwa watumishi wanaofanya kazi ya ukaguzi wa rasilimali hizo katika kituo cha Kibaha.
Kuhusu operesheni Nzagamba awamu ya pili iliyotekelezwa kipindi cha mwezi Oktoba na Novemba, Mpina amesema operesheni hiyo imedhihirisha kuwa, usimamizi thabiti wa sheria, kanuni na taratibu katika sekta ya mifugo, unaweza kuleta tija kwa kuongeza uzalishaji bora wa mazao ya mifugo ambayo ni malighafi ya viwanda.
Katika hatua nyingine, Mpina alizitaka mamlaka zinazotoa Leseni kwa wafanyabishara wanaosafirisha mifugo nje ya nchi kuweka utaratibu rafiki utakaosaidia kundi hilo kutoa mchango wake katika ujenzi wa Taifa na kuondoa au kupunguza vitendo vya biashara ya magendo.
Leave a comment