JOTO la mauaji ya mwandishi wa habari Jamal Khashoggi, Raia wa Saud Arabia limeendelea kupanda na sasa, Rais Donald Trump anatakiwa ‘kumlaani’ Mohammed Bin Salman kwa kile kilichoelezwa kuhusika kwake. Vyombo vya kimataifa vinaripoti…(endelea).
Chama cha Republican nchini Marekani, kimeeleza kwamba hakuna shaka yoyote kuwa, mwanamfalmehuyo wa Saud Arabia, amehusika kwenye mauaji ya mwanahabari huyo.
Maseneta nchini Marekani wanaamini kuwa, Bin Salman amehusika kwenye mauaji hayo licha ya Rais Trump kumtetea na kuonya kuwa, suala hilo linaweza kuvuruga uhusiano wa Marekani na Saud Arabia.
Hatua ya maseneta hao kukubaliana na kuhusika kwa Bin Salman imekuja ikiwa ni baada ya kufanyika kikao cha siri na Mkuu wa Shirika la Ujasusi la Marekani (CIA), Gina Haspel.
Maseneta hao wanaeleza kuwa, mtu yoyote anayeamini kuwa Bin Salman hajahusika kwenye mauaji hayo, mtu huyo ni kipofu wa kujitakia.
Seneta wa mwenye ushawishi mkubwa kutoka chama cha Republican Lindsey Graham amesema anaamini kwamba, bin Salman alihusika katika kupanga njama ya kumuua Khashoggi.
Seneta huyo wa jimbo la Carolina Kusini amesema, bin Salman ni “chizi” na “mtu hatari,” Khashoggi aliuawa ndani ya ofisi za ubalozi mdogo wa Saudi Arabia jijini Istanbul, Uturuki Oktoba 2.
Mwenyekiti wa masuala ya nje wa seneti Bob Corker wa Republican anasema kuwa, kama Bin Salman akifunguliwa kesi kuhusu mauaji hayo, anaweza kukutwa na hatia ndani ya nusu saa.
Mwanahabari huyo alikuwa ni mkosoaji mkubwa wa sera za Saudia hususani mwanamfalme bin Salman.
Tayari Saudia imewashitaki watu 11 juu ya mauaji hayo, lakini wanakanusha vikali juu ya uhusika wa Bin Salman.
Leave a comment