MHANDISI Deusdedit Kakoko, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari (TPA) amesema, yeye ni miongoni mwa watu wanaochunguzwa katika sakata la kuisababishia hasara serikali. Anaripoti Brightness Boaz, Dar es Salaam … (endelea).
Amesema, tayari baadhi ya wafanyakazi wa bandari wamechunguzwa ikiwa ni pamoja na wanne kurejeshwa kazini huku wakipunguzwa vyeo, 17 kufukuzwa kazi na 10 wanaendelea na mashauri.
Amesema, kesi hiyo ya uhujumu uchumi ina jumla ya mashitaka 28, likiwemo la kuisababishia TPA hasara ya zaidi ya Sh 5.1 Bilioni.
Akizungumza na waandishi wa habari na baadhi ya wahariri jijini Dar es Salaam jana tarehe 20 Januari 2021, Mhandisi Kakoko amesema, hatua hiyo imefikiwa baada ya kupokea maagizo kutoka kwa Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu.
Mkurugenzi huyo amesema, licha ya watumishi hao kuchukuliwa hatua za awali, hata yeye anachunguzwa na kwamba, alishakwenda Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU).
“…ni sahihi kama nimekosea ni lazima niwajibike, ndio utaratibu na niko tayari wala hakuna tatizo,” amesema.
Mkurugenzi huyo amesema, wanaohusishwa kwenye sakata hilo ni pamoja na Valentine Sangawe (40) mhasibu, Leticia Massaro (33) na Christina Temu (37) ambao ni makarani pia Eva Vicent (33) na Joseph Ndulu ambao ni watumishi wa Benki ya CRDB.
“Uchunguzi umeendelea baada ya wao kupisha uchunguzi na tunatumaini kwamba, haki itatendeka. Kama hawana tatizo, wanaweze kurudi kazini,” amesema na kuongeza:
“Mheshimiwa Waziri Mkuu alikua sahihi, wakichunguza na kama kuna tatizo, watachukuliwa hatua kamilifu kulingana na sherria za utumishi wa umma.”
Leave a comment