Friday , 26 April 2024
Home Habari Mchanganyiko Mkurugenzi Misungwi aporomosha mitusi
Habari Mchanganyiko

Mkurugenzi Misungwi aporomosha mitusi

Taswila ya jiji la Mwanza
Spread the love

MRADI wa maji wa zaidi ya Sh. 300 milioni uliojengwa katika Kata ya Fera Wilaya ya Misungwi mkoani Mwanza, umeshindwa kuanza kufanya kazi baada ya kudaiwa kuwa umejengwa chini ya kiwango, anaandika Moses Mseti.

Mradi huo uliojengwa kwa zaidi ya miaka mitano na serikali kupitia halmashauri ya wilaya ya Misungwi, umesababisha wakazi wilayani humo kukosa maji kwa muda mrefu.

Ubovu wa mradi huo uliibuliwa na Baraza la Madiwani wa Halmashauri hiyo lililofanyika chini ya Mwenyekiti wake, Antony Masele, ambapo walimuagiza Mkurugenzi, Eliurd Mwaiteleke, kuhakikisha mradi huo unafanya kazi mara moja.

Mmoja wa madiwani aliyezungumza na MwanaHALISI Online ambaye aliomba kuhifadhiwa jina lake, amesema sababu zinazosababisha mradi huo kushindwa kufanya kazi licha ya kutumia kiasi kikubwa cha fedha ni usimamizi mbovu wa Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo.

Amesema kuwa usimamizi mbovu wa mkurugenzi huyo kwenye miradi ya Serikali unachangiwa na mambo mengi ikiwemo ya uwezo wake kiutendaji katika kuiongoza halmashauri hiyo hivyo mamlaka iliyomteua (Rais John Magufuli) inapaswa kuangalia suala hilo.

“Sisi kama madiwani tuliagiza mradi huo wa maji uanze kufanya kazi na kama hauwezi kufanya kazi tuelezwe kwa sababu mradi huo utanufaisha wananchi wetu, ukiangalia wilaya hii mabomba ya maji kutoka ziwa Victoria yanapita hapa kuelekea Shinyanga, lakini Misungwi hakuna maji safi na salama.

“Usimamizi mbovu wa halmashauri hii ndiyo unasababisha miradi mingi kama huu wa maji kushindwa kutekelezeka kwa wakati, kila mkurugenzi akija anawaza upigaji wa dili hatuwezi kufika kwa hali hii,” amesema mtoa taarifa hiyo.

Mtoa taarifa hizi ameendelea kueleza kwamba, sababu nyingine inayochangia kwa wateule wa rais Magufuli, kushindwa kusimamia miradi unasababishwa na tamaa ya fedha na kufanya kazi kwa mihemko.

Amesema kuwa kwa muda mrefu wilaya hiyo imekuwa ikikabiliwa na ukosefu wa maji safi na salama, lakini mamlaka zinazohusika zimeshindwa kutatua tatizo hilo huku akidai pindi madiwani wanapojaribu kulifuatilia kwa ukaribu huonekana wasaliti.

Mmoja wa Wananchi wa kata ya Fera, Maduhu Masalu, amesema kwa muda mrefu Serikali imekuwa ikiwahadaa kuhusu upatikanaji wa maji na salama, lakini mpaka sasa hawajaweza kunywa maji safi na salama.

Amesema baada ya kuusikia mradi huo tangu mwaka 2010 kuanza kwa ujenzi wake katika kata ya Fera karibu na bandari kavu, walidhani wataanza kunufaika na mradi huo, lakini ni miaka saba sasa upatikanaji wa maji safi na salama imekuwa ndoto kwao.

“Viongozi wa halmashauri (Misungwi) wakipata taarifa kwamba kuna viongozi wakitaifa wanataka kuja Mwanza, ndiyo wanaanza kurekebisha huu mradi huu na ukitoa maji siku moja ndiyo basi tena,” amesema Masalu.

Eliurd Mwaiteleke, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Misungwi, alipotafutwa na MwanaHALISI Online kupitia simu yake ya mkononi haikupokelewa, alipotumiwa ujumbe mfupi wa maneno kuhusu mradi huo ambao haufanyi kazi haukuujibu.

Hata hivyo, baadaye Mkurugenzi huyo alipiga simu mwenyewe, ambapo alianza kwa vitisho huku akimuuliza mwandishi wa habari hizi kwamba ni nani aliyemwambia mradi huo haufanyi kazi.

“Nenda Fera ukaangalie kama maji hayatoki na siyo kuongea vitu ambavyo haujavishuhudia, acheni mambo ya kishenzi , sisi tunasumbuka na mradi huo na tumewarudisha watu waliouharibu wanaourudia kwa gharama zao.

“Tuache kufanya kazi kwa mihemko na hata nikwambie basi mradi huo haufanyi kazi unataka nini na unasemaje? acha kunitafuta ubaya na pia uende Fera ukaangalie mwenyewe kama mradi haufanyi kazi kwani hauna miguu,” amesema Mwaiteleke.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari Mchanganyiko

Wakili: Ukimpa zawadi mwenza marufuku kumpora hata mkiachana

Spread the love  WANANDOA na watu waliko kwenye mahusiano ya kimapenzi, wamekumbushwa...

Habari Mchanganyiko

Majaliwa: Mvua zimesababisha vifo vya watu 155, kuendelea hadi Mei

Spread the love  WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema mvua kubwa za El-Nino...

Habari Mchanganyiko

Exim Bank yatoa  vitanda kwa shule ya Jeshi la Polisi Moshi

Spread the love  BENKI ya Exim imekabidhii  seti ya vitanda kwa Shule...

Habari Mchanganyiko

NBC yakabidhi vitanda Shule ya Polisi Moshi

Spread the loveBenki ya NBC imekabidhi msaada wa vitanda 28 kwa Shule...

error: Content is protected !!