FREEMAN Mbowe, Mwenyekiti wa Chadema na viongozi watano wa chama hicho wamesomewa mashtaka nane katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu likiwemo la kufanya maandamano yaliyosababisha kifo cha Mwanafunzi wa Chuo cha Usafirishaji Tanzania (NIT), Akwilina Akwiline na kurudishwa rumande. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Mbowe na wenzake Dk. Vicent Mashinji, Salum Mwalim, Mchungaji Peter Msigwa, John Mnyika na Esther Matiko, wamesomewa mashtaka yao na Wakili wa Serikali, Faraja Nchimbi mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Wilbard Mashauri na kukosa dhamana hadi Machi 29, mwaka huu, uamuzi wa dhamana utakapotolewa.
Wakili Nchimbi amedai kuwa kosa la kwanza ni kufanya mkusanyiko ama maandamano yasiyo na uhalali, siku ya Februari 16, 2018 katika barabara ya Mkwajuni kwa lengo la kuwaogopesha watu waliokuwepo eneo hilo kwa kuona maandamano ya kuvunja amani.
Amesema kosa la pili ni kuendelea kufanya mkusanyiko usio halali, ambapo linawakabili washtakiwa wote wakidaiwa kutenda kosa hilo Februari 16, 2018 Barabara ya Kawawa maeneo ya Kinondoni Mkwajuni.
Viongozi hao kwa pamoja na watu wengine 12 ambao hawajafikishwa mahakamani wakiwa katika maandamano na mkusanyiko wa vurugu waligoma kutii amri ya kusambaratika na kuvunja mkusanyiko huo uliosababisha kifo cha Akwilina Akwiline na majeraha kwa maofisa wa Polisi.
Wakili Nchimbi amedai kuwa kosa lingine ni kuhamasisha chuki kwa wanajamii isivyo halali, ambalo linamkabili Mbowe, siku Februari 16, 2018 akiwa viwanja vya Buibui Kinondoni, Dar es Salaam akihutubia wakazi wa maeneo hayo alitoa matamshi ambayo yangesababisha chuki kwa jamii.
Kosa lingine linalomkabili Mbowe ni uchochezi na kusababisha chuki katika jamii, ambapo inadaiwa amelitenda Februari 16, 2018, akiwa Uwanja wa Buibui Kinondoni, Dar es Salaam akihutubia wakazi hao alitoa matamshi ambayo yangepelekea chuki katika jamii.
Pia kosa lingine linalomkabili Mbowe ni uchochezi wa uasi, ambapo inadaiwa amelitenda Februari 16, 2018 katika viwanja vya Buibui, Kinondoni, Dar es Salaam alipotoa matamshi ambayo yangepandikiza chuki na dharau kwa wananchi wa Tanzania dhidi ya uongozi uliopo madarakani.
Kosa la saba linamkabili Mbowe ambalo ni ushawishi wa utendekaji wa kosa la jinai, ambalo amelitenda Februari 16, 2018 maeneo ya Buibui Kinondoni, Dar es Salaam, akiwa amejumuika na watu wengine aliwashawishi wakazi wa maeneo hayo na DSM kutenda kosa.
Wakili Nchimbi amedai kosa la nane, linamkabili Msigwa ambalo ni kushawishi raia kutenda kosa la jinai, alilotenda Februari 16, 2018 katika viwanja vya Buibui Kinondoni, Dar es Salaam, ambapo aliwashawishi wakazi wa maeneo hayo na DSM kutembea mbele ya umma wakiwa na silaha.
Baada ya kusomewa mashtaka hayo, washtakiwa wote walikana ambapo Wakili Nchimbi amedai upelelezi wa kesi hiyo umekamilika na anaomba tarehe kwa ajili ya kuwasomea maelezo ya awali.
Hata hivyo, Wakili Nchimbi aliwasilisha maombi kwa mahakama hiyo ili washtakiwa wanyimwe dhamana kwa sababu ya usalama wa umma wa Watanzania.
Leave a comment