VYAMA vya upinzani vimetakiwa kuondoa manung’uniko yaliyojitokeza katika Uchaguzi Mkuu wa 2015, kabla ya kuingia ushirikiano mpya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2020. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ni kauli ya James Mbatia, Mwenyekiti wa Chama cha NCCR-Mageuzi aliyoitoa leo tarehe 24 Juni 2020, jijini Dar es Salaam wakati akizungumza na waandishi wa habari.
Mbatia ambaye aliyekuwa mwenyekiti mwenza wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA), katika Uchaguzi Mkuu wa Mwaka 2015, amesema ‘uchaguzi mkuu 2015 uliacha malalamiko.’
Amesema, tangu uchaguzi huo kufanyika, UKAWA haukuwahi kuketi pamoja kujadili na kutafuta suluhu juu ya dosari zilizojitokeza, badala yake kila mmoja akawa kiburi.
“Kama mnaona kwamba mnaweza kujumuika pamoja, ni vyema kufanya uamuzi sahihi ili kuondoa manung’uniko. Sababu kwenye ule uchaguzi uliopita manung’uniko yalijitokeza mengi na hatukukaa kutathimini kwa nini yaliyotokea, kila mmoja akawa na kiburi, ikawa janga,” amesema Mbatia na kuongeza:
“Yaliyopita si ndwele tugange yajayo, kulalamika ya huko nyuma tunapoteza muda, tunaacha kupeleka Watanzania kwenye njia sahihi ya uchaguzi, sisi tunaomba vyama vingine tulete hoja zetu tujadiliane, tuwekane sawa, tuone njia bora.”
Aidha, Mbatia amevishauri vyama vya siasa vya upinzani vitakavyoungana kushirikiana katika uchaguzi huo, kuchagua wagombea wanaokubalika na wananchi, badala ya kuchagua mgombea kutokana na chama anachotoka.
Mbatia metolea mfano kitendo cha UKAWA kupoteza jimbo la Segerea, baada ya wagombea wa vyama hivyo kugongana na kupelekea mgawanyo wa kura, hali iliyompa ushindi mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Bonnah Kamoli.
“Kama tumeingia tukakae tuzungumze, lakini wananchi wana namna bora, na watu siku hizi wanachagua watu zaidi kuliko chama, unaweza ukawa na chama chenye mtandao mkubwa ukashindwa, mtu ambaye hana mwenyekiti au diwani akashinda ubunge,” amesema Mbatia na kuongeza:
“ Mfano Segerea madiwani walikuwa wa Ukawa mbunge kashinda wa CCM, inatakiwa tuangalie je hapa tunashirikiana vipi?”
Leave a comment