MPANGO wa Paul Makonda, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam kuzuia kuuzwa makontena zaidi ya 20 yaliyoingizwa kwa jina lake kutoka nje, unaelekea kukwama. Anaripoti Regina Kelvin…(endelea).
Ni baada ya Dk. Phillip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango kusisitiza uuzwaji wa makontena hayo haraka.
Waziri Mpango ametoa agizo hilo leo tarehe 27 Agosti, 2018 alipofanya ziara ya kushtukiza katika bandari kavu iliyoko jijini Dar es Salaam.
Makonda amenukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari nchini akilalamikia hatua ya Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kuendesha mnada wa kuuza makontena hayo wiki iliyopita.
Akiwa bandarini hapo Waziri Mpango ameeleza kwa msisitizo kwamba, makontena hayo yanapaswa kupigwa bei haraka licha ya kuwepo kwa malalamiko ya mmiliki wake (Makonda).
Akisisitiza jambo hilo Waziri Mpango amesema kuwa, hatishwi na vitisho vya mwanasiasa huyo na ameapa kusimamia sheria na kanuni za kodi zilizoko hapa nchini.
Amesema lazima fedha za kodi kiasi cha Sh. 1.2 bilioni zinazodaiwa na TRA zinalipwa kwa mujibu wa sheria.
Makontena hayo yamebeba samani mbalimbali ikiwa ni mchango uliotolewa na Watanzania wanaoishi Marekani wanaojulikana kwa jina la Six Region Diaspora Council.
TRA ilipiga mnada makontena hayo ambapo mteja hakupatikana kutokana na kudaiwa kuuzwa kwa bei kubwa (milioni 60) wakati wateja walioendekeza mwisho iwe milioni 30.
Mnada huo unaendeshwa na Kampuni ya udalali ya Yono Action Mart. Hatua ya mnada inatokana na kushindwa kulipiwa kodi ya Sh. bilioni 1.2 zinazodaiwa na TRA baada ya kuwasili nchini.
Leave a comment