KANGI Lugola, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi amesema, anafanya kile atakacho Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Magufuli. Anaandika Dany Tibason, Dodoma … (endelea).
Waziri Lugola ametoa kauli hiyo jijini Dodoma wakati akizungumza na waandishi wa habari katika ukumbi wa mikutano wa wizara hiyo, mara baada ya kumaliza kikao na Menejimenti ya Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) pamoja na viongozi wa Kampuni ya Kimataifa ya Iris Corporation Berhard.
Kwenye mkutano huo Lugola ameipa wiki mbili kampuni hiyo (Iris Corporation Berhard) impe majibu ya kuwa lini italeta mtambo wa kutengeneza kadi ghafi au kiasi cha Dola za Marekani Mil 14 (Tsh. Bil 32).
Lugola alisisitiza kuwa, lazima fedha hizo au mtambo huo upatikane kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano haitakubaliana na mchezo mchafu wa aina yoyote, na pia yeye kama Waziri wa Wizara hiyo anaendelea kutekeleza maagizo ya Rais Magufuli.
“Tumezungumza nao na tumekubaliana nao kwamba tuwape wiki mbili ili bodi ya kampuni hiyo ikakae ifanye maamuzi ya aidha waturudishie fedha zetu au walete mtambo.
“Lakini sisi kama nchi, huu mtambo muhimu sana, bado tuna uhitaji, sisi tungependa baada ya hiyo wiki mbili wafanye maamuzi ya kutuletea mtambo,” alisema Lugola.
Pia amewataka wamiliki wa kampuni zilizolipwa kifisadi fedha za Mradi wa mtambo wa NIDA kujisalimisha jijini Dodoma Agosti 3 mwaka huu wakiwa na mtambo huo vinginevyo warejeshe fedha zilizotumika.
Lugola alitoa agizo kwa aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa NIDA, Dickson Maimu na Mfanyabiashara Jack Gotham kufika ofisini kwake Agosti 3 saa 3:00 asubuhi ili kutoa maelezo yanayojitosheleza yatakayomsaidia kutoa maamuzi sahihi kuhusiana na ufisadi wa fedha zaidi ya bilioni 32 za mtambo huo ambao hadi sasa haujafika nchini.
Lugola alidai kampuni zilizolipwa kifisadi ni pamoja na Gotham International ambayo imelipwa shilingi 2,848,878,659.75, Iris Corporation Berhard ambayo imelipwa 22,919,414,169,84, Gwiholoto Impex inayodaiwa shilingi 946,406,989,00, Sykes Travel Agent 5,979,600,00, Dk Shija Paul Rimoy 27,000,000,00, Aste Insurance 1,206,619.93, na Kampuni ya BMTL 569,192,090,00.
Leave a comment