GODBLESS Lema, Mbunge wa Iringa Mjini anaweza kupishana na mwenyekiti wake (Chadema) Freeman Mbowe, iwapo Biswalo Mganga, Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) ‘atamkomalia.’ Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Mbowe yupo katika gereza la Segerea baada ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kumuhukumu kulipa faini au kutumikia kifungo cha miezi mitano jela kutokana na kesi yake ya uchochezi pamoja na viongozi wenzake wa Chadema.
Biswalo amesema, Lema aliudanganya umma kutokana na kusambaza taarifa za uongo kuhusu mauaji ya watu 14 wilayani Manyoni, Singida.
“Kwa hili lazima nitachukua hatua, hatuwezi kuendelea na upotoshaji na uvunjifu wa namna hii,” amesema Biswalo na kuongeza “halafu watu wanatoka na kusema, wanasiasa wa upinzani wanaonewa wakati wanafanya upuuzi wa namna hii.”
Akizungumza na waandishi wa habari leo tarehe 12 Machi 2020, jijini Dar es Salaam Biswalo amesema, Lema alitoa taarifa za uongo wakati alipohudhuria kwenye mazishi ya Alex Joas, katibu wa chama hicho Jimbo la Singida Mashariki.
Mwili wa Joas ulikutwa umetelekezwa kando ya barabara huku ukiwa na majeraha sehemu za kichwa.
“Mtaziona hatua nitazochukua. Nazifahamu mimi na ofisi yangu, hazitafanyika kwa kificho,” amesema Biswalo na kuongeza nimepitia jalada moja baada ya jingine, nimebaini polisi wamezifanyia kazi taarifa hizo tofauti na maelezo ya Lema.”
Amesema, pamoja na wanasiasa kukata kutumia matukio kisiasa, ni bora kukawa na mipaka akifafanua kwamba wengine vifo vyao vinasababishwa na ajali.
“…kuna marehemu mwingine vifo chao vimesababishwa na ajali ya pikipiki, lakini mheshimiwa Lema katika taarifa yake amesema amechinjwa. Mwingine alishambuliwa na fimbo, mateke na ngumi lakini anataja wamechinjwa, huu ni uongo,” amesema Mganga.
Amesema, serikali inapochukua hatua, ni vema wananchi wakatuelewa na kwamba, taifa hili haliwezi kuendelea kuwa la watu wazushi.
Leave a comment