Saturday , 27 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Katiba ya Jamhuri inasemaje kuhusu kuondolewa CAG?
Habari za SiasaTangulizi

Katiba ya Jamhuri inasemaje kuhusu kuondolewa CAG?

Rais John Magufuli akipokea ripoti ya CAG, kutoka kwa aliyekuwa CAG Prof. Mussa Assad
Spread the love

RAIS John Magufuli amemteua Charles Kichere, kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG). Anaandika Mwandishi Wetu…(endelea).

Uteuzi huo umetangazwa leo tarehe 3 Novemba 2019 na Balozi John Kijazi, Katibu Mkuu Kiongozi. Kichere anachukua nafasi ya Prof. Mussa Assad.

Taarifa ya uteuzi huo imeeleza kwamba, Prof. Assad amemaliza kipindi chake cha miaka mitano kuhudumu kama CAG. Hata hivyo, uteuzi huo umeibua mjadala kuhusu uteuzi wa nafasi ya CAG na ukomo wake kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katiba ya Jamhuri, Ibara 144 ya katiba inaeleza, kuwa CAG anaweza kuondolewa katika madaraka ya kazi yake kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake (ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote) au kwa sababu ya tabia mbaya, au kwa kuvunja masharti ya sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma.

Hata hivyo, kuna utaratibu maalumu wa kumwondoa ambapo Ibara ya 144 (3) inabainisha kuwa, iwapo rais ataona kwamba suala la kumwondoa kazini CAG lahitaji kuchunguzwa, basi atateua Tume Maalum ambayo itakuwa na Mwenyekiti na Wajumbe wengine wasiopungua wawili.

Mwenyekiti na angalau nusu ya wajumbe wengine wa tume hiyo itabidi wawe watu ambao ni Majaji au watu waliopata kuwa Majaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani katika nchi yoyote iliyomo kwenye Jumuiya ya Madola.

Iwapo Tume itamshauri rais, kwamba huyo CAG aondolewe kazini kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya, basi rais atamwondoa kazini.

Soma utaratibu uliowekwa katika Katibu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, neno kwa neno

144.-(1) Bila ya kuathiri masharti mengine yaliyomo katika ibara hii, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu wa Jamhuri ya Muungano atalazimika kuacha kazi yake atakapotimiza umri wa miaka sitini au umri mwingine wowote utakaotajwa na Sheria iliyotungwa na Bunge.

(2) Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aweza tu kuondolewa katika madaraka ya kazi yake kwa sababu ya kushindwa kutekeleza kazi zake (ama kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote) au kwa sababu ya tabia mbaya, au kwa kuvunja masharti ya sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma na hataweza kuondolewa kazini ila kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya (4)

ya ibara hii. (3)

Iwapo Rais anaona kwamba suala la kumwondoa kazini Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu kwa mujibu wa masharti ya ibara hii lahitaji kuchunguzwa, basi katika hali hiyo mambo yatakuwa ifuatavyo:-

(a)    Rais atateua Tume Maalum ambayo itakuwa na Mwenyekiti na Wajumbe wengine wasiopungua wawili. Huyo Mwenyekiti na angalau nusu ya wajumbe wengine wa Tume hiyo itabidi wawe watu ambao ni Majaji au watu waliopata kuwa Majaji wa Mahakama Kuu au Mahakama ya Rufani katika nchi yoyote iliyomo kwenye Jumuiya ya Madola;

(b)    Tume hiyo itachunguza shauri lote halafu itatoa taarifa kwa Rais kuhusu maelezo ya shauri lote na itamshauri Rais kama huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aondolewe kazini kwa mujibu wa masharti ya ibara hii kwa sababu ya kushindwa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania  kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya.

(4) Ikiwa Tume iliyoteuliwa kwa mujibu wa masharti ya ibara ndogo ya

(3) itamshauri Rais kwamba huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu aondolewe kazini kwa sababu ya kushindwa kufanya kazi kutokana na maradhi au sababu nyingine yoyote au kwa sababu ya tabia mbaya, basi Rais atamwondoa kazini.

(5) Ikiwa suala la kumwondoa kazini Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu limepelekwa kwenye Tume kwa ajili ya uchunguzi kwa mujibu wa masharti ya ibara hii, Rais aweza kumsimamisha kazi huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu, na Rais aweza wakati wowote kufuta uamuzi huo wa kumsimamisha kazi, na kwa hali yoyote uamuzi huo utabatilika ikiwa Tume itamshauri Rais kwamba huyo Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu asiondolewe kazini.

(6) Mtu ambaye ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu au aliyepata kuwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu hawezi kuteuliwa kushika au kushikilia madaraka ya kazi nyingine yoyote katika utumishi wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano.

(7) Mashartiya ibara hii hayatatumika kwa mtu yoyote aliyeteuliwa kuwa Kaimu Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

ACT: Waongoza watalii wapate maslahi yao inavyostahili

Spread the loveCHAMA cha ACT-Wazalendo kimeitaka serikali kuhakikisha inasimamia maslahi stahiki ya...

Habari za SiasaTangulizi

Prof. Lipumba ajitosa kuviunganisha vyama vya siasa Burundi

Spread the love  MWENYEKITI wa Kituo Cha Demokrasia Tanzania (TCD), Prof. Ibrahim...

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

error: Content is protected !!