THOMAS Simba, Hakimu Mkuu Mkazi wa Mahakama ya Kisutu, jijini Dar es Salaam, imemtaka Tundu Lissu kufika katika mahakama hiyo tarehe 19 Desemba 2019. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Amri hiyo imetolewa jana tarehe 21 Novemba 2019, Hakimu Simba baada ya mdhamini wake, Ibrahim Ahmed kuieleza mahakama, kuwa Lissu ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa Chadema, amepona.
Mdhamini huo alieeleza mahakama, kwamba amewasiliana na Lissu ambaye alimjibu, kuwa amepona lakini hawezi kurejea nchini kwa kuhofia usalama wake.
Ni baada ya Hakimu Simba tarehe 23 Oktoba 2019, kuwataka wadhamini wa Lissu kupeleka uthibitisho wa afya ya mdhaminiwa wao ambaye yupo nchini Ubelgiji.
“Lissu amesema kwa sasa amepona, ila hawezi kuja Tanzania kuhofia usalama wake,” Ibrahim aliieleza mahakama hiyo jana.
Baada ya kauli ya Ibrahim, kwamba Lissu anahofia usalama wake kurejea nchini, Hakimu Simba alisema ‘hatutaki mambo ya siasa hapa, namtaka Lissu aje hapa mahakamani kesi yake iendelee.”
Hakimu huyo alisema, ifikapo tarehe 19 Desemba 2019, wakati kesi hiyo itatajwa, anataka kumwona Lissu ambaye alikuwa Mbunge wa Singida Mashariki, mbele yake.
Kwenye kesi hiyo, Lissu na wenzake watatu – Simon Mkina, mhariri wa gazeti la MAWIO, Jabir Idrissa, mwandishi wa gazeti hilo na Ismail Mehbob, mfanyakazi wa kampuni ya uchapishaji magazeti Jamana – wanakabiliwa na mashitaka matano mahakamani, likiwamo uchochezi.
Wote wanne, wanatuhumiwa kuandika, kuchapisha na kusambaza taarifa hizo kwenye gazeti la MAWIO la tarehe 14 Januari 2016, kinyume na Sheria ya Magazeti ya Mwaka 2002.
Lissu yupo nje ya nchi akiwa amemaliza matibabu, ni baada ya kushambuliwa kwa risasi tarehe 7 Septemba 2019, akiwa nyumbani kwake eneo la ‘Area D’ jijini Dodoma na kupatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa mkoa huo, kisha alipelekwa Nairobi na baadaye Ubelgiji.
Leave a comment