KIKOSI cha Yanga kesho inatarajia kuikabili Namungo FC, kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kutoka sare kwenye mchezo uliomalizika dhidi ya Azam FC, huku uongozi wa kikosi hicho ukieleza kuwa unahitaji pointi tatu kwenye mchezo huo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Hivi karibuni mashabiki wa klabu hiyo waliwajia juu washambuliaji wao kiasi cha kuwazomea kutokana na kucheza chini ya kiwango hali iliyofanya uongozi wa Yanga kujitokeza hadharani na kuwataka mashabiki kuwa na uvumilivu na kuwasapoti wachezaji wao.
Mchezo huo wa Yanga na Namungo utachezwa kesho majira ya saa 1 usiku kwenye Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, ambapo nahodha msaidizi wa Yanga Juma Abdul anatarajia kurejea uwanjani baada ya kukosekana kwenye mchezo uliopita.
Kuelekea mchezo huyo Afisa Habari na Mhamasishaji wa klabu hiyo, Antonio Nugaz amesema kuwa haina haja ya mashabiki kwa sasa kulumbana wala kubishana kwa kuwa wachezaji nao wanaumia kuona timu inafanya vibaya.
“Kwa lolote linaloendelea na kutokea tujue ni sehemu ya mchezo na wachezaji nao wanatamani kufunga kwa sababu kazi yao walioajiliwa ni kucheza mpira na kufunga, nao pia wanaumia kutokufunga,” alisema Nugaz.
Aidha Nugaz ameongezea kuwa, ipo njia sahihi ya mashabiki kutoa madukuduku yao kwa amani lakini siyo kwa vurugu na kuwataka kuwa wavulivu.
Mchezo huo ambao utakao kuwa wa kuvutia kutokana na timu hizo kupishana kwa alama mbili, ambapo Yanga ikiwa nafasi ya tatu na pointi 56, tofauti alama mbili na Namungo ambayo ipo nafasi ya nne.
Leave a comment