JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia Mohamed Jumaa (37), maarufu maarufu Lardh JM, Mkazi wa Kariakoo, kwa tuhuma za mauaji ya walinzi wawili kwa kuwagonga na lori. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Katika tukio hilo, watu sita walijeruhiwa na kupelekwa hospitalini kwa matibabu zaidi.
Waliouawa ni Eliakim Morali, Mkazi wa Mbezi Beach, Mlinzi wa Kampuni ya Lock Fort Security na Saunkoo Bakari(35), Mkazi wa Buguruni, Mlinzi Binafsi (Baunsa).
Kamanda wa Polisi Kanda hiyo, Jumanne Muliro amesema, tukio hilo limetokea jana Alhamisi tarehe 26 Agosti, 2021 saa 12 jioni eneo la Tungi Wilaya Kigamboni katika kituo cha kuuzia mafuta cha JM Petrol Station.
Amesma, mtuhumiwa aliwaua walinzi hao kwa kuwagonga kwa makusudi na gari lenye namba T 176 CVP aina ya DAF lori lililokuwa na tera ambalo halina namba za usajili.
“Mtuhumiwa alifika katika kituo hicho cha kuuzia mafuta cha JM alichokuwa ana kimiliki kwa ajili ya kuhamisha mali zake lakini alichukua gari lake na kutoka nje ya kituo na ghafla.
Alirudi nalo kwa kasi huku likiwa halina tera na kuwagonga walinzi hao waliokuwa getini na kupelekea kufariki dunia papo hapo na kuwajeruhi watu sita ambao walikimbizwa hospitalini kwa matibabu,” amesema Kamanda Muliro
Kamanda huyo amesema, mtuhumiwa huyo alikuwa na kesi ya madai namba 118/2018 Mahakama Kuu iliyofunguliwa na Benki ya Access baada ya kushindwa kulipa mkopo kwa muda muafaka aliochukua katika benki hiyo.
“…mtuhumiwa alishindwa mahakamani licha ya kukata rufaa mara kadhaa na hatimaye mahakama ilitoa amri ya kuuzwa kwa kituo chake cha kuuzia mafuta maarufu kama JM Petrol Station kilichopo Kigamboni,” amesema na kuongeza:
“Jeshi la Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam linaendelea na uchungunguzi wa kina juu ya tukio hili na mtuhumiwa atafikishwa mahakamani hivi karibuni kujibu tuhuma zinazomkabili.”
Leave a comment