Kamishna wa Uhifadhi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), Richard Kiiza amesema kazi kubwa iliyofanywa na Rais Samia Suluhu Hassan imeongeza kasi ya watalii wanaotembelea Hifadhi ya Ngorongoro. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Amesema kutokana na juhudi hizo hadi kufikia mwishoni mwa Desemba 2023 jumla ya watalii 534,065 wametembelea hifadhi hiyo ambapo wageni kutoka nje ni 335,340 na wageni kutoka ndani ya nchi ni 198,725.
Aidha, amesema katika kipindi hicho cha nusu mwaka zaidi ya Sh 123 bilioni zilikusanywa na kuingia kwenye mfuko mkuu wa Serikali.
Akizungumza na waandishi wa habari amesema watalii wamekuwa wakitembelea Ngorongoro kwa idadi kubwa na hivyo kuongeza wigo wa mamlaka hiyo kufanya kazi usiku na mchana ili kusimamia juhudi zilizofanywa za kuutangaza utalii.
Aidha, Kamishna Kiiza ametoa wito kwa watanzania kuendelea kutembelea Hifadhi ya Ngorongoro ili kujionea vivutio mbalimbali ambavyo vipo ndani ya hifadhi na hivyo kutoa fursa kwa wananchi kujifunza kuhusu uhifadhi wa rasilimali za nchi.
Kamishna huyo wa Uhifadhi ameongeza kuwa Uongozi wa NCAA utaendelea kuboresha miundombinu ya utalii ndani ya hifadhi ili kuhakikisha kuwa wageni wote wanaotembelea hifadhi hiyo wanapata huduma nzuri kwa wakati.
Leave a comment