RAIS Dk. Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi wachape kazi hususan katika sekta ya kilimo ili serikali ipate mapato ya kutosha akisema zama za kutegemea misaada ya wafadhili zimepitwa na wakati. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Wito huo umetolewa leo tarehe 16 Oktoba 2023 na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, akizindua daraja la Msingi, lililoko katika Wilaya ya Mkalama, mkoani Singida.
“Limeni kwa wingi tupate fedha kwa wingi tuendeshe mambo yetu na huko ndiko kujitegemea ndugu zangu, wakati wa tumeomba hajatupa mambo hayaendi… umeondoka, sasa hivi hakuna bwana nipe akakupa, sasa fanya kazi niuzie nikulipe. Ndivyo tunavyokwenda sasa na ndiyo uchumi wa dunia ulivyo. Twendeni tukachape kazi kwa bidii,” amesema Rais Samia.
Amesema, Serikali yake inaendelea kuongeza fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji, kutoa ruzuku za mbolea na pembejeo za kilimo, ili kuongeza uzalishaji katika sekta hiyo.
Rais Samia amewatoa hofu wakulima kuhusu masoko ya mazao yao, akisema Serikali yake inaendelea kutafuta masoko nje ya nchi.
“Wananchi ingieni mashambani tanueni mashamba tuzalishe zaidi, masoko serikali tunajitahidi kutafuta na baadhi ya mazao bei ilikuwa iko chini lakini mwaka huu na mwaka jana bei zimejikongoja ziko vizuri zaidi,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia amezitaka halmashauri zitumie mapato yake ya ndani katika kuwahudumia wananchi wake badala ya kutegemea fedha kutoka serikali kuu.
Rais Samia ametoa agizo hilo baada ya wilaya ya Mkalama, kuiomba Serikali itoe fedha kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya afya viwili.
“Mmesema vituo vya afya viwili vifanyiwe ukarabati na hapa ndio ninaposema halmashauri zenyewe zijitutumue lakini kama Serikali kuu tunalichukua na kulifanyia kazi. Tutaona kiasi gani tuweke serikali kuu na kwa kiasi gani halmashauri iweze ili vituo vifanyiwe ukarabati viweze kutumikia wananchi,” amesema Rais Samia.
Leave a comment