ASKARI wa Jeshi la Madagascar wenye silaha wamevamia kambi ya timu ya soka ya Tanzania ‘Taifa Stars’ wakitaka kuwachukua kwa nguvu wachezaji watatu wakidai wana maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Wachezaji hao ni Nahodha, Mbwana Samatta, kipa namba moja Aishi Manula pamoja na beki kitasa Bakari Mwamnyeto.
Tukio hilo, limetokea asubuhi ya leo Jumapili, tarehe 14 Novemba 2021, kwa askari hao kuvamia hotel waliofikia Stars na kusababisha taharuki kwa watu mbalimbali wakiwamo viongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Msemaji wa TFF Cliford Mario Ndimbo akizungumza kwa simu na MwanaHALISI Online amesema, baada ya kupimwa “watu wane walikutwa na corona wakiwemo wachezaji hao watatu.”
“Katika hali isiyo ya kawaida na kinyume cha taratibu za FIFA, askari wenye silaha wamevania kambi yetu hapa hotelini. Tumezuia wasichukuliwe kwani tumefanya vipimo upya na tunasubiri majibu,” amesema Ndimbo.
https://twitter.com/Mwanahalisitz/status/1459791831433105412
Hayo yamejiri saa chache zimebaki kabla ya Stars yenye pointi saba kushuka dimbani nchini humo kuvaana na Madagascar kuanzia saa 10:00 jioni kukamilisha mchezo wa kundi J wa kuwania kufuzu kombe la dunia nchini Qatar 2022.
Madagascar inashika mkia wa kundi hilo ikiwa na pointi tatu huku vinara wakiwa Benin yenye pointi 10 ambao wao watacheza na wanaoshika nafasi ya pili DR Congo yenye pointi nane.
Mshindi wa Benin na DR Congo atasonga mbele hatua inayofuata na iwapo watatoka sare ya aina yoyote, Benin watasonga mbele.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI TV, MwanaHALISI Online na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa mbalimbali
Leave a comment