MWANASHERIA mahiri nchini na Wakili wa kujitegemea, Boniface Mwabukusi amekamatwa na jeshi la Polisi. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Taarifa kutoka vyanzo mbalimbali, akiwamo Askofu Emmaus Mwamakula zinasema, Mwabukusi amekamatwa katika maeneo ya Mikumi, mkoani Morogoro. Anatuhumiwa kwa uchochezi.
Mwabukusi alikuwa mmoja wa wanasheria waliofungua kesi ya kupinga mkataba uliofungwa kati ya serikali na Dubai.
Kukamatwa kwa Mwabukusi kumekuja muda mfupi baada ya Mkuu wa Jeshi la Polisi kuutangazia ulimwengu, kwamba “kuna njama za kumuangusha Rais wa Jamhuri, Dk. Samia Suluhu Hassan.”
Akiandika kupitia mtandao wake wa kijamii, Askofu Mwamakula anasema,
“Taarifa zilizotufikia hivi punde ni kuwa wakili msomi Boniface Kanjunjule Mwabukusi, amekamatwa na Jeshi la Polisi kule Mikumi, Morogoro akiwa pamoja na Katibu wa Kanda wa CHADEMA, Emmanuel Masonga.
“Walikuwa safarini kuelekea Dar es Salaam pamoja na Mdude ndipo wakazuiwa Mikumi.
“Alikamatwa Mdude saa 10 usiku na baadaye maelekezo yakaja ya kukamatwa na wao pia. Mwabukusi ametujulisha kwa simu kuwa wao wameelezwa wamekamatwa kwa tuhuma za uchochezi na simu zao zimechukuliwa.
“Wakili Mwabukusi ndiye aliyesimamia kesi ya kupinga mkataba wa Bandari iliyofunguliwa Mahakama Kuu Kanda ya Mbeya.”
Leave a comment