KANISA la Evangelism Asembless of God (EAGT) imetoa miezi mitatu kuanzia leo tarehe 16 Julai mwaka huu kwa Mchungaji yeyote atakayetaka kurejea baada ya mgogoro kumalizika, sharti aandike barua kwa uongozi na kukiri kosa lake na kuomba msamaha. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea)
Hayo yameelezwa na Askofu Mkuu wa Kanisa hilo Dk Brown Mwakipesile leo tarehe 16 Julai, 2022, jijini Dodoma na kueleza kuwa mwisho wa kupokelewa ni tarehe 20 Octoba 2022.
Akiendelea kutoa maelezo Askofu Mkuu Dk.Mwakipesile amesema kuwa kwa wale ambao watataka kuondoka EAGT, Baraza la Waangalizi limetamka kwamba lazima waheshimu katiba ya EAGT toleo la 2011 Ibara ya IX ambayo inasema,”Mtumishi aachapo utumishi wake EAGT ataondoka pekee pasipo washirika wala mali za Kanisa”.
Amesema kuwa Kanisa la EAGT litaendelea kudumisha amani ya nchi kama ambavyo limekuwa likifanya siku zote.
“Kanisa la EAGT litaendelea kudumisha amani na utulivu katika kutekeleza majukumu yake kwa busara pamoja na hekima itokayo juu kwa maongozi ya Roho Mtakatifu kwani ndiyo msingi wa kanisa letu,” amesema.
Ametumia fursa hiyo pia kuwahimiza Watanzania wote kushiriki katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi ya Mwaka 2022 inayotarajiwa kufanyika tarehe 23 Agosti, 2022.
“Ni zoezi muhimu kwa kila mmoja wetu kuhesabiwa ambapo tunaamini itaisaidia Serikali kuendelea kuweka mipango mbalimbali ya kimaendeelo kwa kujua idadi ya watu wake” amesisitiza Dk.Mwakipesile.
Kanisa Evangelistic Assemblies Of God Tanzania (EAGT) lilikuwa likikabiliwa na mgogoro wa muda mrefu takriban miaka 6 uliotokana na aliyekuwa Makamu Askofu Mkuu wa kanisa John Stephene Mahene kupinga kuondolewa madarakani.
Makamu huyo aliondolewa kwa sababu zinazotajwa kuwa ni kukiuka miongozo ya imani ya kanisa hilo.
Pia alishutumiwa kwa ubadhilifu wa fedha na mali za kanisa uliofanywa na viongozi wa kanisa.
Mwisho.
Leave a comment