‘COUPLE’ maarufu wa Bongofleva, William Lyimo ‘Billnass’ na Faustina Mfinanga ‘Nandy’ leo tarehe 16 Julai, 2022 wamefunga ndoa takatifu katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Mbezi Beach jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ndoa hiyo iliyovuta hisia za wadau wengi wa burudani, imeshuhudiwa Nandy akimwaga machozi wakati akila kiapo cha maisha na mwenziwe.
Nandy alionekana kila muda akifuta machozi hata ulipofika muda wa kutamka maneno ya kiapo hicho, alijikuta akiyasoma kwa kwikwi.
Katika Ibada hiyo ambayo pia ilioneshwa mubashara na kituo kimoja cha runinga, umati mkubwa ulioshiriki ni ndugu wa karibu wa familia zote mbili.
Wawili hao ambao penzi lao limepitia milima na mabonde, kwa mujibu wa Nandy walifungua ukurasa wa mapenzi mwaka 2016 katika ziara ya tamasha la Fiesta.
Hata hivyo, baadae penzi hilo lilizima kama mshumaa baada ya Nandy kudaiwa kutoka na kigogo mmoja kabla ya mwaka 2021 wawili hao kutangaza kurudiana rasmi na penzi kuchipua upya.
Leave a comment